Featured Post

WANAFUNZI JITEGEMEE SEKONDARY WATAKIWA KUTUMIA MITANDAO YA KIJAMII KWA AJILI YA KUJIFUNZIA

 Gwaride la ukakamavu la wanafunzi wa kidato cha tano wa Shule ya Sekondari ya Jitegemee JKT Mgulani likipita mbele ya mgeni rasmi katika hafla iliyofanyika shuleni hapo jijini Dar es Salaam jana.
 Gwaride lilipita jukwaa kuu.
 Meza kuu ikitoa Saluti  wakati gwaride likipita mbele yao.

 Maofisa wa Jeshi wakiwa kwenye hafla hiyo.
 Mmoja wa makamanda wa gwaride hilo, Ibrahim Mrisho akipongezwa na mgeni rasmi baada ya kupokea zawadi yake. Ibrahim alikuwa miongoni mwa makanda sita waliozawadiwa kwa kufanya vyema kwenye gwaride hilo, wengine ni Moses Peter, Azan Mohamed, Kidali Saidi na Clementina Joseph.
  Mkuu wa Shule ya Sekondari Jitegeme, Robert Kessy akizungumza
 Kanali Emanuel Mwaigobeko ambaye ni Mkuu wa Shule ya Sekondari Makongo inayomilikiwa na jeshi akimpongeza mgeni rasmi Mgombolwa kwa hotuba nzuri aliyoitoa kwa wanafunzi waliohitimu mafunzo ya ukakamavu.
 Gadi ya wasichana ikiwa imetulia wakari wa hafla hiyo.
 Mgeni rasmi akipiga saluti wakati akipokea heshima wakati gwaride hilo lililopita mbele yake.
Brass Bendi ya JKT iliwajibika ipasavyo wakati wa kufungwa kwa mafunzo hayo ya ukakamavu.

Na Dotto Mwaibale
KANALI wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), Anchila Kagombola ambaye ni Mkurugenzi wa Ustawi wa Jamii wa Jeshi la Kujenga Taifa Makao Makuu jijini Dar es Salaam, amewaasa wanafunzi kutumia mitandao ya kijamii kwa ajili ya kujifunza na siyo kutumiana jumbe zisizofaa zinazoweza kuhatarisha maisha yao.
Kagombola aliyekuwa mgeni rasmi kwenye sherehe ya kufunga mafunzo ya ukakamavu ya Kidato cha Tano kwa wanafunzi wa Shule ya Sekondari Jitegemee JKT High School 2017, alitoa rai hiyo jana.
Akizungumza katika hafla hiyo, Kagombola aliwapongeza wanafunzi wa Jitegemee kwa kujiunga na shule hiyo inayotoa elimu bora na kusisitiza ukakamavu, maadili, uzalendo,umoja na nidhamu kwa jumla.
Kanali Kagombola, amewaasa wanafunzi hao watumie mitandao ya kijamii kwa kujifunza na siyo kutumiana jumbe hatarishi kwa ajili ya usalama wao na usalama wa taifa.
“Aidha, niwahusie wanafunzi wote wa shule hii kuwa mkwepe vishawishi vyote vya ujana, msome kwa bidii, muache kutazama nafsi zenu hasa watoto wangu wa kike na kupata faraja, kwani zaweza kukatisha ndoto zenu, hivyo muwakatae wote wanaowashawishi kuingia kwenye mienendo hatarishi, mfano kufanya ngono, utumiaji wa madawa na vitendo vya uhalifu.
Aidha, mitandao kama Facebook, Twitter, WhatsApp, Youtube na mingine itumike kwa ajili ya kujifunza, siyo kutumiana jumbe hatarishi kwenu na kwa usalama wa nchi. Tafadhali sana, mmenisikia?”
Kagombola ametoa pongezi kwa Mkuu wa Shule ya Sekondari ya Jitegemee, Luteni Kanali Robert Kessy kwa kuendesha mafunzo hayo ya ukakamavu kwa wanafunzi wa kidato cha kwanza, kidato cha tano na kwa wahamiaji.
Alibainisha kuwa katika mtazamo wa nje mafunzo ya ukakamavu huonekana hayana umuhimu kwa walengwa, lakini yanasaidia vijana kuishi kwa nidhamu wawapo shuleni na uraiani na bila tabu yoyote.
“Faida  za mafunzo haya ya ukakamavu ni pamoja kudumisha nidhamu, utimamu wa mwili, uwezo wa kufikiri haraka, uvumilivu, uadilifu, kujiamini na suala zima la kutenda na kuamua kwa wakati ili kupata matokeo mazuri katika masomo,” alisema Kagombola.
Hata hivyo, ameomba mpango wa kutoa mafunzo ya ukakamavu mashuleni uliokuwepo miaka ya nyuma urejeshwe ili kujenga ukakamavu , uzalendo na wanafunzi kuwa na maadili.
Pia aliwasisitiza wazazi na walezi kuhakikisha mtoto wa kike anapatiwa  elimu bora kwa kuwa ndio walezi wa jamii.
Akizungumzia mafunzo hayo,Luteni Kanali Kessy alisema yalianza 1985 na kwamba wakati huo yalikuwa yakichukua wiki mbili sasa wiki tatu na yanafanyika baada ya muda wa masomo.
‘Mafunzo haya ya ukakamavu yalianzishwa ili kuwafanya wanafunzi wawe wazalendo, wakakamavu, wenye maadili na nidhamu.
Gwaride hilo la wanafunzi wa kidato cha tano liliongozwa na Gwaride Kamanda, ambaye ni mwanafunzi  aitwaye Zulfa Ally likihusisha wanafunzi 256 na gadi nane.

(Imeandaliwa na mtandao wa www.habari za jamii.com-simu namba 0712727062)

Comments