- Get link
- Other Apps
Featured Post
Posted by
Unknown
on
- Get link
- Other Apps
Na Agness Moshi – MAELEZO
Ulaji wa nyama una faida lukuki kwa
afya ya binadamu ikiwa ni pamoja na upatikanaji wa virutubisho vya aina ya
protini ambayo ni rahisi kutumika mwilini, madini mbalimbali (Calcium,
Magnesium, Phosphorus, Zinc na Chuma); vitamini aina ya folic asidi, E, B
na B12 ambayo inapatikana katika nyama pekee.
Nyama pia inasaidia katika ukuaji na
kuongeza afya ya mlaji kutokana na uwezo
mkubwa wa kujenga mwili, kukarabati seli za mwili zilizokufa, kuzalisha
chembe hai mpya, kurekebisha kinga ya mwili, kuongeza damu na kuimarisha
mifupa.
Hata hivyo faida zote hizo
zinapatikana tu, kwa walaji wa nyama iliyo bora na yenye kiwango. Hivyo ni
vizuri wananchi wakazingatia kanuni za ulaji wa nyama yenye kiwango ili
kujiepusha na athari zinazoletwa na nyama isiyo na kiwango.
Msajili wa Bodi ya Nyama Tanzania
(TMB) Bi.Suzana
Kiango amesema kuwa nyama yenye kiwango na bora huanzia kwenye utunzwaji
wa mifugo wenye kuzingatia kanuni za
uzalishaji bora, unenepeshaji wa mifugo yenye umri mdogo kwa kuwalisha chakula
mchanganyiko kwa muda usiopungua siku 90 kabla ya kuchinja.
Bi.Kiango amesema kuwa hatua
nyingine ni katika uchinjaji ambapo inashauriwa ufanyike kwenye machinjio bora
ambayo yanakidhi viwango vya usafi. Hii ni pamoja na kuwa na sakafu na kuta
zinazosafishika, maji ya kutosha na sehemu za kuning’iniza wakati wa kuchuna na
kupasua.
“Kanuni za uchinjaji ni pamoja na
kupumzisha mifugo ili kuipoteza fahamu na kumfanya mnyama asiogope na kuzalisha
asidi nyingi inayosababisha nyama kuwa ngumu, pia iwe rahisi kutoa damu yote
katika misuli. Uning’inizwaji wa chune mara baada ya kuchinjwa unasaidia
kuondoa damu iliyo mwilini. Endapo damu haitatoka yote kwenye chune
itasababisha nyama kuwa na rangi nyeusi na kuharibika mapema”, alisema
Bi.Kiango.
Madhara ya ulaji wa nyama isiyo na
viwango na bora ni pamoja na kupata magonjwa ya tumbo, kuharisha na kutapika
endapo nyama itapata vimelea vya magonjwa hayo, kuugua magonjwa ya kuvimba
miguu, kifua kikuu, shinikizo la damu, kisukari na kansa.
Hata hivyo, Bi. Kiango
amesisitiza kuwa magonjwa haya yanaweza kuwatokea pia watu ambao hawatumii
kabisa nyama kwa hivyo si nyama pekee ndio chanzo cha magonjwa haya japo
inaweza kuwa sababu ya mtu kuugua.
“Bodi imeendelea kutoa elimu kwa watumiaji na
wachinjaji wa nyama kupitia vyombo mbalimbali vya habari kama vile, redio,
televisheni na magazeti. Pia katika maonesho mbalimbali kama Saba saba na Nane
nane ambapo wataalamu wa bodi hutoa elimu kwa wananchi wanaotembelea mabanda
ikiwa ni pamoja na kusambaza vipeperushi” amesema Bi.Kiango.
Namna nyingine ya kutoa elimu ni
pamoja na kutumia matamasha ya nyama choma, wiki ya mayai na maonesho ya kuku,
wiki ya chakula salama na siku ya chakula duniani. Wakati wa shughuli hizi
wanashiriki hupatiwa elimu kuhusu faida na athari za kula nyama isiyo na
viwango ili kunusuru afya zao.
Aidha walaji huelekezwa maeneo
mbalimbali wanayoweza kupata nyama hiyo, na kwa upande wa
wafanyabiashara wa nyama hupewa maelekezo ya kuboresha miundombinu ya
kuzalisha, kuchinja na kuuza kwa kuzingatia viwango vya ubora na usalama.
Kutokana na baadhi ya
wafanyabiashara ya nyama kuendelea kuwauzia walaji nyama isiyo na viwango kwa
kujua au kutojua madhara ya nyama hizo, Bi.Kiango alisema kuwa
Bodi inachukua hatua za kuhakikisha wafanyabiashara hao wanapata
uelewa wa kutosha.
“Bodi imeanza kutoa mafunzo kwa
watumishi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa ambao watashiriki katika kutekeleza
majukumu ya Bodi ikiwa ni pamoja na kusimamia uzalishaji wa nyama na
kuelimisha wachinjaji ,walaji na wadau wengine wanaojishughulisha na
uzalishaji wa nyama”alifafanua Bi.Kiango.
Aliendelea kusema mafunzo hayo
yameshatolewa kwa vitendo kwa watumishi wanne kutoka katika kila Mamlaka za
Serikali za Mitaa za mikoa ya Dar es Salaam, Pwani, Morogoro na Dodoma ambapo
hadi sasa jumla ya wadau 490 katika maeneo tajwa wamekwisha patiwa elimu hiyo.
Pia mafunzo yanatolewa na wadau wengine ambao ni Chuo cha nyama cha VETA, Dodoma
na Kampuni ya nyama ya jijini Arusha.
Comments
Post a Comment