Featured Post

MHANDISI MATHEW MTIGUMWE AWASHUKURU WADAU WOTE WALIOSHIRIKI MAONESHO YA KILIMO – NANE NANE 2017

Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo Mifugo na Uvuvi (Kilimo) Mhandisi Methew Mtigumwe
 
Na Mathias Canal, Dar es Salaam
Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo Mifugo na Uvuvi (Kilimo) Mhandisi Methew Mtigumwe anawashukuru wananchi, wadau wa kilimo na Taasisi mbalimbali kwa kushiriki Maonesho ya Kilimo na Sherehe za Wakulima – Nane Nane mwaka 2017, ambapo maadhimisho kwa ngazi ya Ki-Taifa yalifanyika katika Uwanja wa Maonyesho ya Kilimo wa Ngongo, Manispaa ya Lindi.

Aidha, maadhimisho ya Ki-Kanda yalifanyika katika viwanja vya maonyesho ya John Mwakangale –Mbeya; Mwalimu J.K. Nyerere –Morogoro; Themi – Arusha; Nzuguni - Dodoma; na Nyahongolo – Mwanza.

Akizungumza na mtandao wa www.wazo-huru.blogspot.com Mhandisi Mtigumwe amesema kuwa Maonesho ya mifugo sanjari na Maonesho ya Kilimo yametoa changamoto na kuleta mapinduzi katika Ufugaji, Uvuvi, na Kilimo na kutoa ajira hususani kwa vijana kwa kuwaongezea zaidi kipato na kuondoa umasikini. 

Mtigumwe alisema kuwa Wizara, taasisi/Makampuni ya umma na binafsi, Mabenki na wadau wote wa kilimo na mifugo wataendelea kuwasaidia wakulima na wafugaji hapa nchini ili kuongeza uzalishaji kuwezesha upatikanaji wa malighafi kwa ajili ya viwanda vinavyokusudiwa kuanzishwa.

''Ni matumaini yangu  kuwa elimu ya matumizi ya teknolojia mbalimbali kwa wadau wengi kwa muda mfupi imetolewa ipasavyo lakini pia wadau walijionea na kujifunza huduma zitolewazo na serikali, mashirika ya umma na binafsi''

''Katika Maonesho hayo Teknolojia/Bidhaa mbalimbali zilionyeshwa ikiwa ni pamoja na zana za Kilimo, Mbegu bora za mazao mbalimbali, Uzalishaji wa mazao katika mazingira yaliyodhibitiwa ambapo pia Taasisi za kitafiti zilionyesha teknolojia mbalimbali za kuongeza tija zenye ukinzani dhidi ya magonjwa mbalimbali, Utengenezaji wa chanjo dhidi ya magonjwa ya mifugo, Uboreshaji wa viasilu ili kupata mifugo na mazao ya kilimo yanayostahimili hali ya hewa kutokana na maeneo walipo wananchi wanaohitaji kujihusisha na ufugaji na kilimo na udhibiti wa magonjwa'' Alisema Mtigumwe
   
Teknolojia na Bidhaa zingine zilizoonyeshwa ni pamoja na uzalishaji bora wa mazao ya nafaka, ubunifu wa teknolojia rahisi za kutotoa mayai, Kuongeza thamani mazao ya mifugo, Makampuni ya mawasiliano, ambapo Taasisi za elimu zilionyesha ubunifu wa kumsaidia mfugaji, Tiba za asili, Wasindikaji wakubwa na wadogo wa mazao ya Kilimo, Mifugo, Uvuvi, Asali, na Nta.

Sikukuu ya wakulima inayofahamika kuwa Nanenane husherekewa nchini kote kuanzia 1 Agosti mpaka tarehe 8 Agosti kila mwaka. Sherehe hiyo inatayarishwa na kuratibiwa na Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi na kuhusisha Taasisi, Wizara na mtu mmoja mmoja wanaoshughulika na kilimo.

MWISHO

Comments