- Get link
- Other Apps
Featured Post
KAMUGISHA: TANZANIA YA VIWANDA ITAFANIKIWA TUKICHANGIA MAENDELEO YA SAYANSI KAMA TUNAVYOCHANGIA HARUSI
Posted by
Unknown
on
- Get link
- Other Apps
Mkurugenzi Mtendaji na Mwanzilishi Mwenza
wa Shirika la Young Scientist Tanzania (YST), Gosbert Kamugisha, akizungumza na
wanahabari (hawapo pichani) kuhusu Maonyesho ya Sita ya Wanasayansi Chipukizi
yanayotaraji kuanza Agosti 8 mpaka 9, 2017 katika Kituo cha Kimataifa cha
Mikutano cha Julius Nyerere (JNICC) jijini Dar es Salaam. Kulia ni Mkurugenzi Mtendaji
wa Royal Dutch Shell Afrika Mashariki ambaye pia ni Mkurugenzi wa BG Tanzania,
ambayo ni kampuni tanzu ya Shell, Marc den Hartog.
Mkurugenzi Mtendaji wa Shell Afrika
Mashariki na BG Tanzania, Marc den Hartog, akizungumza na wanahabari kuhusu
udhamini wa kampuni yake katika Maonyesho ya Wanasayansi Chipukizi Tanzania ambayo
yanalenga kuandaa kizazi cha magwiji wa sayansi nchini.
Muasisi Mwenza na Mkurugenzi wa Ushauri
wa Masuala ya Sayansi wa Shirika la YST, Joseph Clowry, akizungumzia mafanikio
ya tasisi hiyo ndani ya miaka sita tangu ianze kuendesha maonyesho hayo.
Meneja Uhusiano wa Nje kutoka kampuni ya
BG Tanzania, ambayo ni kampuni tanzu ya Royal Dutch Shell, Patricia Mhondo,
akifafanua jambo juu ya udhamini wa kampuni hiyo katika kuwawezesha wanasayansi
chipukizi nchini Tanzania.
Na Daniel Mbega, MaendeleoVijijini Blog
MALENGO ya kuona Tanzania ya Viwanda yatafanikiwa ikiwa
jamii itawekeza katika kuchangia maendeleo ya elimu ya sayansi kwa wanasayansi
chipukizi ili kuwapata wataalam wengi zaidi.
Kuliko kuchangia sherehe za harusi zinazogharimu fedha
nyingi kwa tukio la mara moja, ni vyema wanajamii wakachangia fedha hizo kwa
watoto wao kujifunza masomo ya sayansi ambayo yataleta tija kwa jamii na taifa
kwa ujumla.
Hayo yameelezwa jijini Dar es Salaam leo hii na Mkurugenzi
Mtendaji na Mwanzilishi Mwenza wa Shirika la Wanasayansi Chipukizi Tanzania
(Young Scientists Tanzania – YST), Dkt. Gosbert Kamugisha, wakati akizungumza
na wanahabari kuhusu maonyesho ya sita ya wanasayansi hao chipukizi
yanayotarajiwa kuanza Agosti 8 – 9, 2017.
“Wanajamii tunachanga fedha nyingi kwa ajili ya sherehe za
harusi, lakini tunashindwa kuwekeza kwenye sayansi na teknolojia ambako ndiko
uliko msingi mkubwa wa maendeleo ya taifa lolote.
“Siyo ajabu ukakuta tunachangia shilingi laki moja hadi laki
tano kwa ajili ya kuburudika kwa vinywaji na vyakula kwenye sherehe ya siku
moja tu, lakini watoto wetu hawa maskini wanahitaji walau hata shilingi elfu
hamsini tu kuwaendeleza kwenye masomo ya sayansi. Ni vyema tubadilike ili
tuweze kuifikia ndoto ya kuona Tanzania ya Viwanda,” amesema Dkt. Kamugisha.
Dkt. Kamugisha amesema kwamba, malengo ya serikali ya awamu
ya tano ya kuifanya Tanzania kuwa nchi ya viwanda yatatimia ikiwa tu wananchi
watabadili mtazamo wa kuchangia maendeleo ya sayansi na teknolojia na akawaomba
wadau kuunganisha nguvu ili kuwaandaa wanasayansi chipukizi.
“Tunaweza kuanzisha viwanda vingi, lakini kama hatutakuwa na
msingi imara wa wataalam wa sayansi na teknolojia itakuwa ni kazi bure,”
amesema Dkt. Kamugisha na kuongeza kwamba, uwepo wa wanasayansi wengi utasaidia
hapo baadaye kufanya kazi na kuviendeleza viwanda hivyo vitakavyoanzishwa
kutimiza azma ya serikali.
Amesema ni muhimu kuwekeza kwa wanafunzi ambao wanaonyesha
kuvutiwa na masomo ya sayansi kwani wao ndiyo watakaoendesha viwanda siku za
usoni.
Maonyesho ya sita
Kuhusu maonyesho ya sita ya YST, Dkt. Kamugisha amesema
mwaka huu yatashirikisha jumla ya wanafunzi 200 na walimu 100 kutoka shule 100
za sekondari za Tanzania – Bara na Visiwani.
Maonyesho hayo yanatarajiwa kufanyika katika Kituo cha
Kimataifa cha Mikutano cha Mwalimu Julius Nyerere (JNICC) jijini Dar es Salaam
ambapo pia yatashuhudia wanafunzi waalikwa 850 wakihudhuria kutoka shule
mbalimbali za Dar es Salaam.
Dkt. Kamugisha amesema kwamba, tangu walipoanzisha maonyesho
hayo miaka sita iliyopita wameshuhudia mafanikio makubwa ambapo wanafunzi
katika shule nyingi wamehamasika kupenda na kuchukua masomo ya sayansi tofauti
na ilivyokuwa miaka ya nyuma
“Ingawa bado kuna uhaba wa walimu, lakini shule nyingi
ambazo zimepata kushiriki maonyesho haya zimeonekana kufanya vizuri zaidi
kwenye masomo ya sayansi ikilinganishwa na shule ambazo hazijapata kushiriki,”
amesema.
Ameipongeza serikali kutokana na juhudi kubwa inazozifanya
hivi sasa za kupeleka vifaa mbalimbali vya maabara katika shule nyingi za
sekondari na kuwapa fursa wanafunzi ya kujifunza kwa vitendo.
Hata hivyo, amesema kuwa kazi nyingi zinazoletwa kwenye
maonyesho hayo siyo zile zinazoandaliwa kwenye maabara tu, bali ni za ubunifu
wa wanafunzi wenyewe katika mambo mbalimbali ya kijamii na kutafuta namna ya
kukabiliana na changamoto hizo.
"Maeneo yanayoguswa ni afya, kilimo, usalama wa
chakula, mawasiliano, nishati na mazingira, elimu, usalama katika usafirishaji
na mengine yanayogusa jamii," amesema.
Ameongeza kusema kwamba, ingawa wamekuwa wakizitembelea shule
nyingi za sekondari kuwafundisha na kuwaelekeza walimu na wanafunzi namna ya
kubuni kazi za kisayansi na teknolojia, lakini kwa sasa inaonekana mwamko ni
mkubwa kwa shule nyingi kiasi kwamba hata maombi ya ushiriki yamevuka kiwango.
“Awali tulianza na shule sita tu na tulikuwa tunakwenda
kuwaomba washiriki, lakini hivi sasa katika shule nyingi kunakuwepo na
ushindani wa wanafunzi wenyewe ambapo huchaguliwa wanafunzi wawili ambao wazo
lao linakuwa bora zaidi ili washiriki kwenye mashindano ya kitaifa,” amesema.
Udhamini
Kwa miaka mitano sasa mashindano hayo yamekuwa na wadhamini
mbalimbali huku mdhamini mkuu akiwa kampuni ya British Gas (BG) ambayo ni
kampuni tanzu ya Royal Dutch Shell.
Kufuatia udhamini huo, wanafunzi na walimu wote wanaoshiriki
maonyesho hayo huwa hawachangii gharama yoyote kuanzia nauli za kuwatoa
mikoani, malazi na chakula, gharama ambazo hulipwa kupitia udhamini huo.
“Tunaishukuru sana BG Tanzania kwa kufanikisha maonyesho
haya na tunawaomba wadhamini wengine wajitokeze zaidi ili tuendelee kuwaandaa
wanasayansi chipukizi kwa ustawi wa taifa letu,” amesema Dkt. Kamugisha.
Kwa upande wake, Mwanzilishi Mwenza wa YST, Joseph Crowry
kutoka Ireland, amewaomba Watanzania kuhamasika na kuwaendeleza watoto wao
katika masomo ya sayansi ili kuwajengea msingi imara.
Amepongeza jitihada za vyombo vya habari katika kuhamasisha
maonyesho hayo kila mwaka, lakini akaomba jitihada hizo ziendelee zaidi ili
kujenga msingi imara wa wanajamii kupenda sayansi.
“Kule Ireland tumekuwa na maonyesho kama haya kwa zaidi ya
miaka 50 sasa na kwa hakika, kila maonyesho yanapofanyika jiji la Dublin
husimama kila mtu akiwa na shauku ya kwenda kutazama kazi za ubunifu wa sayansi
na teknolojia,” amesema Crowry.
MaendeleoVijijini
inafahamu kwamba Ireland imepiga hatua kubwa sana katika sayansi kiasi kwamba
makampuni makubwa ya teknolojia na mitandao, ikiwemo Google, yameweka makao yao makuu huko.
Mkurugenzi Mtendaji wa Royal Shell Afrika Mashariki ambaye
pia ni Mkurugenzi wa BG Tanzania, Marc den Hartog, amesema kampuni hiyo
imevutiwa kufadhili mashindano hayo kwa kuwa ni mradi unaolenga kuwajenga
wanasayansi.
“Ni mradi mzuri mno ndiyo sababu hatuoni hasara kuwekeza
fedha nyingi katika hili, tunataka tuwe na wanasayansi, wabunifu na watalaam wa
teknolojia wa kutosha,” amesema.
Comments
Post a Comment