- Get link
- Other Apps
Featured Post
Posted by
Maendeleo Vijijini
on
- Get link
- Other Apps
Na Daniel Mbega, MaendeleoVijijini
JIMBO la Colorado nchini Marekani linasemekana ndilo lenye
uchumi unaokua kwa kasi zaidi kuliko majimbo mengine yote 51 yaliyobakia.
Ukuaji huo unasemekana unatokana na kitendo cha Serikali ya
jimbo hilo kuhalalisha matumuizi ya bangi na mimea kama hiyo tangu Januari 2014.
Kwa sasa jimboni humo maduka ya kuuza bangi na mimea kama
hiyo yanaingiza jumla ya Dola 295 milioni 295 (sawa na Shs. 649 bilioni za
Tanzania) huku Serikali ikipata jumla ya Dola 51 milioni (sawa na Shs. 112.2 bilioni
za Tanzania) kama kodi ya mapato.
Hata hivyo, bangi pamoja na mihadarati mingine imepigwa
marufuku sehemu nyingi duniani ikiwemo Tanzania kwa sababu inahatarisha afya za
watu na kuathiri nguvu kazi.
Licha ya kupigwa marufuku kimataifa, lakini bangi na dawa
nyingine za kulevya zimetamalaki na biashara hiyo ndiyo inayoongoza kwa mapato
makubwa kati ya biashara zote haramu duniani.
Biashara ya dawa za kulevya inafanywa na watu wakubwa wenye
mitandao imara, yakiwemo makundi hatari ya kihalifu, kwani fedha zinazotokana
na biashara hiyo ndizo zinazotumika kufadhili makundi ya kigaidi ulimwenguni,
kuvuruga chaguzi mbalimbali kwa kuwaweka watu wanaowapenda ambao watalinda
maslahi yao, zinatumika pia kuleta machafuko katika nchi zenye rasilimali ili
wakati serikali zinapambana na waasi, wao watakuwa wanachota rasilimali hizo
kiulaini.
Makundi haya yana nguvu za ajabu na yamepenya katika taasisi
nyingi nyeti. Kwa maana hiyo, ni rahisi ‘kuwashughulikia’ wote wenye viherehere
ambao wanataka kukwamisha biashara zao.
Wakati Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paulo Makonda,
alipotangaza rasmi operesheni ya kuwakamata vigogo wa dawa za kulevya alikuwa
na nia nzuri tu ya kuendeleza mapambano yaliyokubaliwa na serikali nyingi
duniani.
Lakini hakujua kwamba, alikuwa ameingia kwenye anga za
miungu-watu wasioguswa (The Untouchable Godfathers), ambao kwa miaka mingi
wameimarisha mtandao wao hapa Tanzania.
Orodha aliyopewa Makonda haina tofauti kubwa kama ile ambayo
ilipelekwa Ikulu mwaka 2006 na kundi la viongozi wa dini ikiwataja vigogo wote
wa dawa za kulevya wakiwemo wanasiasa, wafanyabiashara na viongozi wa dini.
Haina tofauti na ile ambayo imekuwa ikitajwa na wafungwa wa
Kitanzania walioko Uchina na Hong Kong ambako wanatumikia adhabu mbalimbali
vikiwemo vifungo vya maisha kutokana na kukamatwa na dawa za kulevya wakiwa
kama ‘punda wabeba mizigo’ (drug mules).
Licha ya orodha hizo kutolewa kitambo, hakuna kiongozi
yeyote mwenye dhamana aliyewahi kuthubutu kulivalia njuga suala hilo kwa
utekelezaji, na kwa kadiri miaka inavyosonga mbele, orodha hiyo imeendelea kuwa
ndefu ikiwataja hadi watoto wa vigogo wa serikali na wafanyabiashara
tunaowaheshimu katika jamii.
Makonda, akifanya kazi kwa niaba ya Serikali ya Awamu ya
Tano chini ya Rais Dk. John Magufuli, alikuwa na nia njema ya kuonyesha
utendaji wa serikali katika masuala mazito ambayo yamewashinda viongozi wengi,
lakini hakujua kwamba wahusika kwenye mtandao huo wana mkono mrefu na wanaweza
siyo tu kumharibia kazi na maisha yake, bali kuivuruga operesheni nzima na
ikakosa maana.
Leo hii Makonda anaumia kwa mashambulizi mfululizo ambayo
yamefichua mambo yake binafsi yaliyofichika kwa sababu ya uthubutu wake katika
kupambana na dawa za kulevya.
Hakujua kwamba, lile kundi la watu waliohisi kubanwa na
Siasa ya Ujamaa na Kujitegemea wakati wa Mwalimu Julius Nyerere, lilikuwa
limejiimarisha Tanzania tangu mwaka 1992 walipoliua Azimio la Arusha kule Zanzibar
na kuleta Azimio la Zanzibar la ‘Soko Huria’ ambalo lilizaa ubepari uchwara.
Ni ubepari huo uchwara ambao katika kipindi cha miaka
zaidi ya 20 tangu kuuawa kwa Azimio la Arusha tumeshuhudia matabaka mbalimbali
yalivyowaathiri Watanzania. Waliokuwa viongozi enzi za Mwalimu, ambao walijiona
wamebanwa, wakatumia fursa hiyo kujilimbikizia mali, wakauza kila kitu,
wakaruhusu na mifumo mingine kutamalaki, japo kwa siri, na kuibariki kwamba
ndiyo inayofaa.
Rushwa, ambayo katika kipindi cha Mwalimu ilikuwa msamiati
mgeni (ingawa ilikuwepo kwa siri), leo hii imetawala na imeundiwa majina mengi
ya kuihalalisha. Wengine wanasema ni takrima, bakhshishi, asante, mlungula,
mshiko na majina mengineyo mengi.
Hii yote imetokana na kuruhusu mfumo hatari wa Mafia
utamalaki, mfumo mbaya ambao kwa sasa ndio unaotumiwa hata kutuchagulia
viongozi wetu, na wahusika wakuu wengi wao wamo katika biashara ya dawa za
kulevya.
Hapa sizungumzii Kisiwa cha Mafia kule Pwani, nazungumzia
kundi lile hatari la Mafia ‘Morte alla
Francia, Italia anela!’ (Kifo kwa Mfaransa ni Kilio kwa Mtaliano),
lililoibuka katika Visiwa vya Sicily, Italia katikati ya karne ya 19 na
kuogopwa na wengi duniani kutokana na vitendo vyao.
Pengine vijana wengi hawalielewi vizuri kundi hili
hatari, lakini niwakumbushe tu kwamba, kundi hili mojawapo ya majukumu yake ni
kuwalinda mafisadi, kusafirisha silaha, kuhujumu mikataba, kutengeneza fedha
bandia, usafirishaji wa dawa za kulevya, ufisadi, fedha chafu, rushwa kwenye
siasa na mambo mengine haramu ikiwemo hata kuua wapinzani wao.
Ni mara ngapi tumeshuhudia mfumo mbovu katika upatikanaji
wa viongozi, ufisadi uliotamalaki, rushwa iliyoota mizizi, mikataba feki na
uporaji wa rasilimali zetu ikiwemo ujangili na usafirishaji wa wanyama hai. Hawa
Mafia ndio wanaohusika.
Mafia, au Cosa Nostra, yaani ‘Kitu Chetu’, ndilo
linaloitesa nchi hii kama tunavyoona mikataba mibovu ya madini, mafuta na gesi,
utaifishaji wa ardhi yetu kwa kisingizio cha uwekezaji na mambo mengine kadha
wa kadha.
Tunashuhudia kashfa za vigogo wengi wa Serikali kuficha
matrilioni ya fedha nje ya nchi, tukio ambalo huko nyuma lilikuwa adimu.
Wanafanya hivi kwa maslahi ya nani? Uzalendo umekwenda wapi? Ni aibu kubwa.
Chaguzi mbalimbali zimegubikwa na wimbi la rushwa na
ufisadi, tunapata viongozi kwa njia haramu na baadaye tunatambua kwamba,
viongozi hao wamewekwa na kambi fulani, ili baadaye watetee maslahi ya kambi
hiyo na ikiwezekana kufumbia macho vitendo vya kihalifu viendelee. Haya yote
yanatuthibitishia kwamba Mafia iko miongoni mwetu, ndiyo inayoweka mashinikizo
ya kuwapata viongozi.
Leo hii tunachaguliwa viongozi, yaani watu wanapitishwa
madirishani ili watuongoze, bila ridhaa yetu. Kinachofanyika ni kwa kundi hili
kuwaandaa watu ambao lenyewe linadhani watalitumikia kwa maslahi yao.
Na limefanikiwa sana, tunaona zoezi la ubinafsishaji
lilivyoua mashirika ya umma ingawa tunasadikishwa kwamba ni shinikizo la
Shirika la Fedha Duniani (IMF) na Benki ya Dunia, lakini dhahiri limefanywa kwa
manufaa ya kundi fulani likiwahusisha na viongozi.
Tazama kashfa ya EPA ambayo tunaona kampuni nyingi za
mifukoni ndizo zilizochota mabilioni ya fedha, na tunaelezwa kwamba fedha hizo
ndizo zilizotumika kuwapitisha baadhi ya viongozi kupitia ‘dirishani!’
Badala ya kuwashughulikia ipasavyo ikiwemo kutaifisha
mali zao, tukaona jinsi watu hao walivyoelezwa ‘kishkaji’ kwamba warejeshe
wenyewe fedha hizo. Wengi hawakushtakiwa mpaka leo.
Kumbuka pia kashfa ya Tegeta Escrow ambayo iliwahusisha
hadi vigogo wa Ikulu waliochota mamilioni ya fedha huku wakitumia viroba
kubebea.
Huku mitaani wapo
watu wengi ambao ‘wana ubia’ na viongozi wa Serikali kiasi kwamba wamekuwa kama
miungu-watu. Hawaguswi, na ukiwasogelea watakwambia ‘viongozi wote wa serikali
wako chini yao’!
Nyerere aliweza
kuidhibiti hali hiyo alipomweka ndani yule Giriki aliyekuwa akitamba kwamba
“Serikali yote iko mfukoni mwake”. Lakini kwa sasa hakuna awezaye kufanya
hivyo, kwa sababu “Wote wametenda dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu!”
Tumeruhusu wenyewe
kuwa na ‘koo’ za akina ‘Gambino’, ‘Bonanno’, ‘Piana dei Greci’ ‘Francesco
Cuccia’ na wengineo, na tutaendelea kushuhudia viongozi wakipitishwa
madirishani kutuletea ‘tuwathibitishe’ ikiwa wale waliopo walipitia madirishani
pia.
Hii ni hatari, ndugu
zangu, na siyo ajabu katika siku zijazo tukasikia viongozi wetu wanaamrishwa
wasifanye hiki ama wafanye hiki na kundi kama hilo. Si tumekubali wenyewe kuwa
watumwa wa Mafia!?
Nyerere
alionya kuhus hali hiyo mwaka 1995 alipowaasa wanaCCM na Watanzania wote kwamba
tujihadhari na fedha za bangi ambazo zilikuwa zimelenga kutumika ili ‘mtu wao’
apitishwe na CCM kuwania urais katika uchaguzi wa kwanza wa vyama vingi.
Natambua wapo wengi, hata kwenye uongozi wa Serikali hii
ya Awamu ya Tano, ambao wanaendelea kumchukia Mwalimu Nyerere kwa sababu ya
siasa zake. Na wanamchukia kwa mengi.
Mara kadhaa wapinzani wa falsafa za Mwalimu wamekuwa
‘wakilazimika’ kumtaja ‘Baba wa Taifa’ pale tu wanapotaka kupigiwa makofi
kwenye mikutano mbalimbali, ili waonekane wamesema jambo jema, lakini mioyoni
mwao wamejaa unafiki na uzandiki na wanamchukia mno.
Kwahiyo,
Makonda alijua anafanya kazi ya kizalendo kabisa, lakini badala yake anaonekana
amejipalia makaa kwenye kazi na maisha yake binafsi kiasi kwamba hivi sasa ana
hofu kubwa moyoni.
Mafia wa
Tanzania wana mtandao mrefu. Nakumbuka lile sakata la mbunge mmoja ambaye
kupitia kampuni yake ya uwindaji mwaka 2009 aliomba kibali cha kuwinda
pundamilia 600! Inaelezwa kwamba alikuwa amepewa mkataba wa kusafirisha nyama
ya pundamilia hao kwenda Mashariki ya Kati.
Ninakumbuka
jinsi kwa mwaka 2011 Jeshi la Polisi lilikamata shehena kubwa kubwa za dawa za
kulevya ambapo hadi kufikia Septemba lilikuwa limekamata jumla ya kilogramu 483
za dawa za kulevya mchanganyiko aina ya heroine na cocaine.
Miongoni
mwa waliokamatwa mwaka huo alikuwemo mchungaji mmoja wa Kanisa la Lord Chosen
Charismatic Church lililopo Kinondoni Biafra jijini Dar es Salaam aliyekutwa na
kilogramu 81 za Cocaine nyumbani kwake Kunduchi Mtongani.
Pia watu
watano – Ali Mirzaei Pirbaksh, raia wa Iran; Said Mrisho, mkazi wa Tandale;
Aziz Juma Kizingiti, mkazi wa Magomeni Mapipa; Abdul Mtumwa Lukongo, mkazi wa
Kariakoo na Hamidu Kitwana Karim walikamatwa Septemba 6, 2011 majira ya saa
3:30 usiku eneo la Africana Mbuyuni, wilayani Kinondoni wakiwa na kilogramu 97
za heroine.
Januari 12, 2012 majira ya saa 12:00 asubuhi Polisi
walimkamata Morine Amatus Liyumba pamoja na wenzake katika eneo la Mchinga II
mjini Lindi wakiwa na kilogramu 210 za heroine zenye thamani ya Shs. 6.3
bilioni. Morine alitajwa kuwa binti wa aliyekuwa Mkurugenzi wa Utumishi na Utawala
wa Benki Kuu, marehemu Amatus Liyumba.
Morine ambaye wakati huo alikuwa na miaka 21 tu, alikamatwa
pamoja na mfanyabiashara wa magari, Ismail Adamu au kwa jina lingine, Athuman
Mohamed Nyaubi, 28, raia wa Tanzania anayeishi Afrika Kusini. Mwingine aliyekamatwa
ni dereva, Hemed Said, 27, mkazi wa Mtoni, Temeke, Dar es Salaam ambaye pia ni
mtoto wa mwenye nyumba yaliyokutwa madawa hayo na Pendo Mohamed Cheusi, 67,
mkazi wa Lindi ambaye ni mmiliki wa nyumba hiyo.
Kukamatwa kwa watu hao kulikuja miezi michache tu baada ya
Umoja wa Mataifa (UN), kuonya kuwa Afrika Mashariki imekuwa ikipokea kiasi
kikubwa cha dawa ya heroine kutoka Afghanistan na Iran baada ya ukanda huo
kuibuka njia rahisi ya kusafirisha dawa hizo kwenda Ulaya, Amerika Kaskazini na
sehemu nyingine duniani.
Ripoti hiyo Umoja wa Mataifa ilimesema, wafanyabiashara wa
dawa za kulevya, kwa kukabiliwa na ugumu katika kusafirisha mizigo kupitia Asia
na Mashariki ya Kati, sasa wamegeukia Afrika, hasa Afrika Mashariki kwa kuwa ni
kituo kikubwa cha kusafirisha heroine kwenda Ulaya na sehemu nyingine duniani.
Kukamatwa kwa binti wa Liyumba kuliibua mambo mengi, na
ilielezwa kwamba, huyo alikuwa mmoja tu kati ya watoto wengi wa vigogo ambao
wamekuwa wakihusishwa kwenye biashara hiyo haramu ya dawa za kulevya.
Chanzo kimoja cha habari kilipata kueleza kwamba, wasafirishaji
wa dawa za kulevya wana njia nyingi za kuwakwepa askari ambapo kinachofanyika
ni kwamba kuna mtu anayetumwa kwenda kuchukua mzigo ‘Pele’ (yaani Brazil) au ‘Musharaf’
(yaani Pakistan) kupitia Iran.
“Huyu akishapakia mzigo(dawa za kulevya)anapanda ndege mpaka
may be Dubai au nchi za Kusini mwa Afrika
kama Msumbiji au Afrika Kusini. Huyu mtu akitoka na mzigo Brazil ama Pakistan/Iran
kazi yake inakwisha baada ya kushuka airport ya moja ya nchi za Kusini mwa
Afrika, ambako hashuki ovyo ovyo lazima kunakuwa na mchongo wa kushukia hapo, yaani
mabosi wake wanakuwa wameshaseti mambo hapo airport husika hivyo jamaa anashuka
hapo salama na kuingia mjini then
anachukua hoteli.
“Hapo sasa anatumwa kijana kama huyu wa Liyumba kutoka hapa Bongo
na passport yake ya karatasi anasafiri kwa njia ya barabara anapita boda ya Tanzania
na Msumbiji anagonga passport yake hiyo ya karatasi kama kawaida hapo boda then aningia Msumbiji, anakwenda mpaka
kwenye hiyo hoteli aliyofikia yule aliyetoka shamba, hapo wanabadilisha mzigo na
huyu dogo aliyetoka Bongo anauchukua mzigo then
anatambaa nao kivyake kwa njia ya barabara, anapita pale boda anagonga muhuri
wa kumtoa Msumbiji, huyo anaingia zake Tanzania bila kushukiwa na yeyote kwa
kuwa wanajua alikwenda mara moja tena na passport ya karatasi. Basi anasafiri
mpaka Dar es Salaam anakabidhi mzigo anakula milioni zake 5 kwa safari hiyo ya
siku kama 3 tu! Lengo la kwenda kumpokea yule ni kuficha ile mihuri ya visa za ‘Pele’
au ‘Musharaf’ zisionekane maana visa za nchi hizo zinajulikana na watu wa dawa
za kulevya... Brazil utakwenda kufanya nini kama sio madawa tu..?” kinaeleza
chanzo hicho.
Tukumbuke pia jinsi tembo wetu wanavyopopolewa na
majangili. Ni mara ngapi tumewasikia mawaziri na vigogo wengine wa Wizara ya
Maliasili na Utalii wakitajwa kuhusika kwenye mitandao hiyo? Iliwezekanaje
twiga wetu wakasafirishwa kwenye ndege wakati wapo maofisa wengi kila kona,
wakiwemo wanausalama?
Haitoshi, zipo kampuni ambazo zinatajwa kuwa na uswahiba
na vigogo wa serikali na zimekuwa zikifanya ujangili lakini zinatazamwa tu. Hii
ndiyo mitandao ya ki-Mafia ninayoisema.
Itakumbukwa
kwamba, Machi 2015 Polisi mkoani Arusha walilikamata gari
la Kampuni ya Uwindaji wa Kitalii ya Wengert Windrose Safaris, lenye namba za
usajili T 655 ARR likiwa na shehena ya magunia 11 ya dawa za kulevya aina
ya bangi iliyokuwa ikisafirishwa kwenda nchi jirani ya Kenya. Kampuni hiyo
ilitajwa kuwa na uswahiba na aliyekuwa Waziri wa Maliasili na Utalii wa wakati
huo, Lazaro Nyalandu.
Kwahiyo,
Makonda anaweza kuwa na makosa yake kama binadamu, lakini nguvu kubwa
iliyommaliza ni mtandao wa ki-Mafia uliotamalaki nchini ambao unajihusisha na
biashara nyingi haramu na hautaki kuingiliwa.
Ukiingia
kwenye anga zao watakumaliza – iwe kwa maneno au hata kukupora uhai wako.
0656331974
(Imeandaliwa
na www.maendeleovijijini.blogspot.com)
Comments
Post a Comment