- Get link
- Other Apps
Featured Post
Posted by
Maendeleo Vijijini
on
- Get link
- Other Apps
Na Jovina Bujulu – MAELEZO
Mizigo mikubwa waliyonayo wanawake ni miongoni
mwa changamoto za kijamii ambazo zimekuwa kikwazo kwa wao kushiriki kikamilifu
katika masuala ya siasa.
Hayo yamesemwa na Balozi Getrude Mongella ambaye
pia ni Rais Mstaafu wa Bunge la Afrika alipokuwa akizungumzia ushiriki wa
wanawake katika siasa nchini.
“Changamoto kubwa ni pamoja na teknolojia duni
ambayo inamlazimisha mwanamke kuendelea kulima kwa kutumia jembe la mkono,
kutembea umbali mrefu kutafuta maji, kutafuta kuni na suala zima la kulea
watoto” alisema Balozi Mongella.
Akizungumzia suala la teknolojia duni alisema
kuwa katika nchi zinazoendelea hilo limeendelea kuwa tatizo kubwa na kwa kuwa
wanawake ndio wazalishaji mali wakubwa, wamejikuta wanaweka nguvu zao nyingi
katika matumizi ya jembe la mkono. Hivyo ukulima kwa kutumia jembe la mkono
haukidhi mahitaji yao ya chakula katika familia na kujikuta wamebaki kuwa omba
omba.
Pamoja na changamoto hizo Balozi Mongella
amesema kuwa ushiriki wa wanawake bado ni mkubwa na ameitaka jamii kuwawezesha
kubeba baadhi ya mizigo kwa mfano kuimarisha huduma za afya ya jamii.
Balozi Mongella alitoa ushauri kwa jamii kutokukaa
kimya bali kuzungumzia changamoto hizo na utatuzi wake ikiwa ni pamoja na kuwaelimisha
wanaume, kwani wakielimika na kutumika vizuri baadhi ya changamoto zitaondoka
na kasi ya mwanamke kupiga hatua itakuwa kubwa.
Aidha, alivitaka vyama vya wanawake kuamka na
kuendeleza mapambano ya kumkomboa mwanamke kwani ajenda ya wanawake ni ya kudumu na haijakamilika hata kidogo.
Zaidi ya hayo, Balozi Mongella amewataka
wanawake kutambua nafasi yao katika kuchangia uchumi wa taifa, ili wafike
mahali waonyeshe mchango wao katika Tanzania ya viwanda ambayo Watanzania wanaitaka
na kuwashauri wanawake waliopata elimu kusaidia kuwavusha wanawake wengine.
Naye
Mwenyekiti wa Chama cha ACT-Wazalendo ambaye alikuwa Mgombea Urais pekee
mwanamke katika uchaguzi uliopita wa 2015, Mama Anna Mgwira alisema wanawake
wakipewa nafasi wanajitoa kwa ukamilifu hivyo aliwataka wasimamie nafasi zao
huku wakifanya kazi kwa weledi, uaminifu, wajiheshimu na wawajibike ili kuondokana
na dhana ya kwamba hawawezi kazi bila kusimamiwa na kusaidiwa.
Comments
Post a Comment