- Get link
- Other Apps
Featured Post
TALIRI: TAASISI KONGWE YA UZALISHAJI NA UTAFITI WA MIFUGO BORA ILIYODHAMIRIA KUWAKOMBOA WAFUGAJI NCHINI
Posted by
Maendeleo Vijijini
on
- Get link
- Other Apps
KILOMETA mbili kutoka stendi ya mabasi
Mpwapwa, upande wa kaskazini, kuna taasisi muhimu sana kwa ustawi na maendeleo
ya mifugo nchini Tanzania, MaendeleoVijijini
inaandika.
Taasisi hii ambayo kwa zaidi ya miongo 11
imepitia majina mengi, kwa sasa inaitwa Taasisi ya Utafiti wa Mifugo Tanzania
(Tanzania Livestock Research Institute – Taliri), ambayo imekuwa kitovu cha
uzalishaji na utafiti wa mifugo nchini.
Yawezekana wafugaji wengi hawaijui taasisi
hii, lakini kwa wale wachache ambao wanaifahamu wameweza kunufaika nayo
kutokana na mifugo bora inayopatikana hapo pamoja na kuelekezwa mbinu bora za
ufugaji wenye tija.
MaendeleoVijijini imetembelea mara kadhaa taasisi hiyo inayopatikana katika
Latitude 60° 20’Kus na Longitude 36° - 30° 30’Mash mjini Mpwapwa katika Mkoa wa
Dodoma, yapata umbali wa kilometa 430 kutoka Dar es Salaam na kilometa 112
kutoka Dodoma mjini.
Aidha,
taasisi hiyo iko umbali wa kilometa 17 kutoka stesheni ya Gulwe kwenye Reli ya
Kati na kilometa tano kutoka uwanja wa ndege wa Ilolo, ambako hata hivyo
hakujawahi kutua ndege yoyote kwa zaidi miaka 10 sasa.
Ukifika
katika taasisi hiyo utashangaa wakati utakapokutana na majengo ya mawe ambayo
Dk. Eligy Mussa Shirima, Mkurugenzi Mkuu wa Taliri, anasema yalijengwa zaidi ya
miaka 100 iliyopita na hayajawahi kupata ufa.
Jengo la Utawala la Taliri-Mpwapwa ambalo lilijengwa na Wajerumani tangu mwaka 1905.
“Majengo
mengi unayoyaona, likiwemo hili la utawala, yalijengwa na Wajerumani tangu
mwaka 1905… humu ndani tumefanya maboresho tu kwa kuweka terazo (tiles), paa na dari
nzuri, vinginevyo yako imara mno,” anasema Dk. Shirima.
Makao
makuu ya Taliri yapo katika kituo hicho cha Mpwapwa ingawa yamekuwa
yakihamishwa mara kwa mara.
Taasisi hiyo ilianzishwa na wakoloni wa
Kijerumani mwaka 1905, kikiwa kama kituo cha utafiti wa mifugo ambapo
kiliendelea mpaka baada ya Vita Kuu ya Kwanza ya Dunia. Aidha, walijenga na
josho la kuogeshea wanyama mwaka 1907, ambalo ndilo kongwe kuliko yote Afrika
Mashariki.
Josho lililojengwa na Wajerumani mwaka 1907 ambalo linatumika mpaka leo.
Kabla ya kuhamia katika eneo la Kikombo
kilipo hivi sasa, kituo hicho kilikuwa kimenzishwa mwaka 1903 katika Kijiji cha
Godegode, takriban kilometa 20 kutoka Mpwapwa mjini.
Sababu za kuhamishia kituo hicho mjini
Mpwapwa, kwa mujibu wa Dk. Eliakunda Kimbi, ambaye ni Mkurugenzi wa Kituo cha Taliri-Mpwapwa
ambacho ni miongoni mwa vituo saba vya utafiti vilivyo chini ya Taliri, ni
baada ya kushuhudia farasi na ng’ombe wao wengi wakifa kwa magonjwa ambayo
hawakuwa wameyafahamu, hivyo kuamua kuanza utafiti.
“Baadaye ikagundulika kwamba wanyama hao
walikuwa wakifa kwa ugonjwa wa Sotoka (Rinderpest), hivyo wakajenga josho la
kuogeshea wanyama mwaka 1907. Josho hilo ndilo kongwe kuliko yote Afrika
Mashariki,” anasema Dk. Kimbi.
MaendeleoVijijini imebaini kwamba, sababu za Wajerumani kuhamishia kituo hicho
Mpwapwa, hasa katika eneo la mlimani, ni kutokana na mazingira yake tulivu
ambayo yamelifanya eneo hilo kuwa tofauti na maeneo mengine ya Mkoa wa Dodoma
ambao ni nusu-jangwa.
Eneo
la shamba kubwa kilipo kituo lipo katika mwinuko wa meta 1,100 kutoka usawa wa
bahari, wakati shamba jingine lililopo Kiboriani liko kwenye mwinuko wa meta
1,750 na shamba la chakula cha mifugo la Ilolo liko kwenye mwinuko wa meta 900
kutoka usawa wa bahari.
MaendeleoVijijini inatambua kwamba, wastani wa mvua kwa mwaka kwenye eneo
hilo ni 660mm na hutofautiana kutoka mwaka hadi mwaka ambapo pia kuna miaka
inayokuwa na ukame wa muda mrefu. Asilimia 90 ya mvua hunyesha kati ya Desemba
na Aprili, ingawa kunakuwepo na kipindi cha ukame mwezi Februari, kama ilivyo
katika maeneo mengi ya mikoa ya Dodoma na Singida. Wastani wa chini wa joto ni
nyuzijoto 15.5°C, na Agosti ndio mwezi wenye baridi sana (13.8°C). Wastani wa
kiwango cha juu cha joto ni nyuzijoto 27.5°C, huku mwezi Novemba ukiwa na joto
kali (30.2°C).
Udongo
ni wa tifutifu uliochanganyika na kichanga hasa kwenye maeneo ya miteremko,
wakati kwenye maeneo ya mabonde kuna udongo wa mfinyanzi. Udongo wote huo una
kiwango kidogo cha naitorojeni na fosforasi ingawa madini ya potasiamu ni
mengi. Udongo huu wote una kiwango cha kati ya pH 5.3 hadi 8.6 huku eneo hilo
likiwa limetandwa na misitu ya miombo, mahogany, na mingineyo.
Aidha,
MaendeleoVijijini
inafahamu kwamba, mazingira tulivu ya eneo hilo, na shughuli zilizokuwa zikifanywa
na Wajerumani, vilikifanya kituo hicho kuwa miongoni mwa maeneo ambayo
Waingereza waliyashambulia hasa mwaka 1916 wakati wa Vita Kuu ya Kwanza ya
Dunia, wakidhani Wajerumani walikuwa akificha silaha nzito.
Shughuli kuu za kituo wakati huo
Dk. Kimbi anasema kwamba, mnamo mwaka 1922
wakoloni Waingereza walianza kukihudumia kituo hicho na kuanzisha Maabara ya
Utafiti wa Magonjwa ya Mifugo (Veterinary Pathology Laboratory).
Kuanzia mwaka 1924 hadi 1929 shughuli kuu
za kituo hicho zikawa utafiti wa magonjwa ya Sotoka na Ndigana (Rinderpest and
Trypanosomiasis), lakini sasa utafiti huo ukawa unafanyika kwa wanyama wote
waliokuwepo kituoni hapo na maeneo ya jirani kwa vile ilionekana magonjwa hayo
yalikuwa yakiwashambulia na wanyama wengine mbali ya farasi.
Zaidi ya dozi 50,000 za kuzuia Sotoka
(anti-rinderpest serum) zilitolewa kila mwaka.
Makao makuu ya Idara ya Sayansi ya Mifugo
na Utunzaji wa Wanyama, kama ilivyojulikana wakati huo wa ukoloni, yakahamia
Mpwapwa kutoka Dar es Salaam mwaka 1929.
Aidha, uboreshaji wa ng'ombe wa kienyeji
wenye asili ya Iringa, Rungwe, Singida na Masailand ulikuwa umeanza mapema
mwaka 1923.
“Kuanzia mwaka 1930 hadi 1938, utafiti wa
utunzaji wa mifugo ulipata sura mpya baada ya kuletwa mtaalam wa madawa na
malisho. Shughuli za uzalishaji wa mifugo zilipamba zaidi mwaka 1944 baada ya
kuteuliwa mtaalam wa vijinasaba (geneticts). Taasisi Kuu ya Mifugo ikaanzishwa
mwaka 1951, na wakati huo huo kituo kikaona umuhimu wa kuiendeleza sekta ya
mifugo, hivyo kikaanzisha kituo cha mafunzo ambacho sasa kinajulikana kama
Livestock Training Agency (LITA),” anasema.
Ni katika kipindi hicho ambapo Shaaban bin
Robert (jinale la asili ni Shaaban bin Selemani), mtu mashuhuri katika historia
ya Tanganyika hasa katika kuikuza lugha ya Kiswahili, alifanya kazi kituoni
hapo.
MaendeleoVijijini imefika mpaka katika
nyumba ambayo Shaaban Robert aliishi na ofisi aliyofanyia kazi, pamoja na
kushuhudia minazi miwili kati ya mitatu ambayo aliipanda wakati huo.
Nyumba ambayo Shaaban Robert bin Selemani aliishi miaka ya 1950 wakati akifanya kazi katika Idara ya Mifugo ya Wakoloni.
Jengo ambalo lilitumiwa kama ofisi hata enzi za Shaaban Robert.
Dk. Kimbi anasema, makao makuu ya idara
hiyo yalirejeshwa Dar es Salaam mwaka 1954 na kumwacha Ofisa Mkuu wa Mifugo
hapo Mpwapwa ambaye alisimamia Maabara ya Utafiti, Kituo Kikuu cha Uzalishaji,
na Utafiti wa Mifugo na Malisho.
Wanyama wa kufugwa waliokuwepo kituoni hapo
walikuwa ng'ombe, nyati, kondoo, mbuzi, nguruwe, kuku na farasi.
Mnamo mwaka 1962 kulikuwa na mabadiliko ya
muundo wa wizara na kukifanya kituo hicho kiitwe Kituo cha Majaribio ya Mifugo
kikiwa kinahusika na mambo ya kilimo, utunzaji wa mifugo na uvuvi.
Mwaka 1966 Sera ya Maendeleo ya Mifugo
iliyopitishwa na Bunge ikiwa inasisitiza umuhimu wa kueneza ng'ombe wenye ubora
wa juu vijijini ilikifanya kituo kikazanie uzalishaji wa ng'ombe, ambapo sasa
kikajulikana kama Kituo cha Uzalishaji wa Mifugo (Livestock Breeding Station).
Mwishoni mwa miaka ya 1960 kituo hicho kikaitwa tena Taasisi ya Utafiti na
Mafunzo ya Mifugo kikiegemea zaidi maendeleo ya mifugo.
Kuanzia mwaka 1977 utafiti wa mafunzo na
mifugo viligawanywa katika taasisi mbili tofauti, Taasisi ya Utafiti, ambayo
kuanzia Julai 1981 ilijulikana kama Taasisi ya Uzalishaji na Utafiti wa Mifugo
(LPRI) ikiwa chini ya Mkurugenzi na Chuo cha LITA kikawa chini ya Mkuu wa Chuo.
Shirika la Utafiti wa Mifugo Tanzania (Taliro) lilianza kusimamia taasisi hiyo
mwaka 1981 hadi lilipokufa mwaka 1989, na kuanzia hapo mpaka sasa taasisi hiyo
pamoja na chuo viko chini ya Wizara inayoshughulikia mifugo japo imekuwa
ikibadilishwa kila mara.
Hivi sasa taasisi hiyo inajishughulisha na
uzalishaji wa ng'ombe aina ya Mpwapwa, Mbuzi wa Maziwa jamii ya Malya (Malya
Blended Goat), Kuku wa Kienyeji, Malisho, Lishe, Matibabu ya Mifugo, na Utoaji
wa Elimu kwa Wakulima na Wafugaji.
Taliri inasimamia jumla ya vituo saba
vilivyoko katika agro-ikolojia tofauti nchini, ambavyo ni: Mpwapwa na Konga
(Dodoma), Mabuki (Mwanza), Naliendele (Mtwara), Uyole (Mbeya), Tanga (Tanga),
na West Kilimanjaro (Kilimanjaro).
Kituo cha Taliri-Mpwapwa na shughuli zake
Kimsingi,
Taliri yenyewe imetokana na kituo hiki cha Mpwapwa, na ndiyo maana hata makao
makuu yako hapo.
MaendeleoVijijini imeelezwa kwamba, Kituo
cha Utafiti Mpwapwa kina raslimali mbalimbali, ikiwemo raslimali watu, ardhi na
mifugo. Mpaka sasa kituo hicho kina watumishi 72 waliopo katika ajira ya kudumu
na malipo ya uzeeni, hekta 8,556 za ardhi (zikijumuisha hekta 6,614 za shamba
kuu la Kikombo, hekta 1,800 za shamba la Kiboryani na hekta 142 za shamba la
Ilolo ambalo ni kwa ajili ya chakula cha mifugo), ng’ombe 853, mbuzi 309 na
kuku 120.
Dk.
Eliakunda Kimbi anasema, tafiti zinazofanyika hivi sasa kituoni hapo ni pamoja
na: Utafiti wa ng’ombe aina ya Mpwapwa wanaofaa kwa maziwa na nyama unaolenga
kuhifadhi aina hiyo ya koosafu, kuzalisha idadi ya kuwatosheleza kwa ajili ya
wafugaji na kuimarisha kizazi (purity maintenance and stabilization).
Pia
wanafanya utafiti wa ng’ombe bora wanaoweza kuzalisha maziwa mengi na wanaoweza
kustahimili nyanda kame ambapo wanatumia vizazi vya Danish Red x Mpwapwa.
Wanatafiti
ng’ombe bora wanaoweza kutoa nyama nyingi na wanaoweza kustahimili nyanda kame
kwa kutumia vizazi vya Beef Master x Boran.
“Tunafanya
utafiti unaolenga kuzalisha ng’ombe bora kwa kutumia viini tete (embryo
transfer). Kwa kipindi cha majaribio tumeshazalisha ndama watano aina ya Bons
Mara kutoka Afrika Kusini. Viini tete hivi vimepandishwa kwa ng’ombe wetu aina
ya Mpwapwa Boran na Mpwapwa,” anasema Dk. Kimbi.
Dk. Kimbi
anasema, wanafanya tafiti za kuhifadhi na kutathmini uwezo wa mifugo ya asili
kutoka kwa wafugaji, miongoni mwa mifugo hiyo ni ng’ombe aina ya Singida White,
Iringa Red na Ufipa pamoja na mbuzi aina ya Gogo White, Newala Goats, na Ujiji
Goats.
MaendeleoVijijini imeelezwa pia kwamba,
taasisi hiyo inafanya utafiti wa aina ya mbuzi mwenye uwezo wa uzalishaji mzuri
wa nyama na maziwa (blended goats) kwenye mazingira ya wafugaji wa Tanzania
ambapo kwa sasa kazi kubwa inayofanyika ni kuzalisha idadi kubwa ya
kuwatosheleza wakulima na kuimarisha kizazi (purity maintenance and
stabilization).
Aidha,
anasema wamefanya utafiti kutathmini uwezo wa uzalishaji wa kuku wa asili kwa
kuangalia aina nne za kuku hao ambao ni Kuchi, Kishingo, Horace na Sasamala.
“Tumefanya
utafiti wa majani na mikunde mbalimbali kwa ajili ya kuongeza upatikanaji wa
mbegu za malisho bora kwa wafugaji ambapo kwa sasa jumla ya aina 80 za malisho
zinahifadhiwa katika hifadhi ya vinasaba vya malisho (Gene Bank) hapa kituoni,”
anasema Dk. Kimbi.
Kwa mujibu
wa mkurugenzi huyo, msimu wa 2015/2016 kituo hicho kilizalisha kiasi cha
malisho (hay) mikate 26,108 ambayo 56% iliuzwa kwa wafugaji na 44% ilitumika
kwa ajili ya mifugo ya kituo.
Dk. Kimbi amebainisha kwamba, wanafanya
utafiti na uzalishaji wa nguruwe bora na kuwasambaza kwa wafugaji, lakini pia
wanafanya utafiti wa vyakula mbadala vya nguruwe unaolenga kupunguza gharama za
uzalishaji.
“Tunafanya utafiti wa mnyororo wa thamani
wa maziwa unaolenga kuboresha ukusanyaji na usindikaji wa maziwa kwa wafugaji
wa nyanda kame.
“Hapa nchini, mradi huu unafanyika katika
wilaya za Chamwino na Manispaa ya Dodoma ambapo unawashirikisha wafugaji 600.
Wadau wengine washiriki ni pamoja na wazalishaji wa maziwa wakubwa, kati na
wadogo, wakusanyaji na wauzaji wa maziwa, wachakataji wa maziwa, walaji wa
maziwa, watafiti na wagani,” anafafanua Dk. Kimbi.
Aidha, Taliri inafanya utafiti unaolenga
kuongeza tija ya uzalishaji wa maziwa kwa wafugaji wadogo hadi wakubwa katika
mikoa ya Tanga, Kilimanjaro, Arusha, Iringa na Mbeya, mradi unaotekelezwa kwa
ushirikiano baina ya Taliri-Mpwapwa, Taasisi ya Kimataifa ya Utafiti wa Mifugo
(ILRI), Chuo Kikuu cha New England – Australia na Chuo Kikuu cha Scotchland
(SURC).
Taliri pia inafanya utafiti wa uendelezaji
na uboreshaji wa kuku wastahimilivu wa mazingira ya Tanzania ambao unafanyika
katika mikoa ya Simiyu, Mwanza, Singida, Dodoma, Mbeya, Njombe, Lindi, Mtwara,
Morogoro na Tanga.
“Mkoani Dodoma, utafiti huu unafanyika
wilaya za Chamwino na Bahi, ambapo kila wilaya mradi umewashirikisha wafugaji
160 na idadi ya kuku waliosambazwa ni 4,400,” anaongeza Dk. Kimbi.
Dk. Kimbi anasema kwamba, wanafanya utafiti
unaolenga kutoa teknolojia bora ya udhibiti wa maambukizi ya minyoo kwa mifugo
na wakati huo huo wanasambaza mifugo bora ya ng’ombe, mbuzi na kuku na malisho
kwa wafugaji na vikundi vya wafugaji kwa ajili ya utafiti na uzalishaji.
Mikakati iliyopo
Ili kutekeleza shughuli mbalimbali za
maendeleo, Taliri imeweka mikakati ya kuendeleza miundombinu ya utafiti na
huduma mbalimbali za ofisi, watumishi na mifugo.
Miundombinu hii ni pamoja na maabara,
miundombinu ya mashamba ya mifugo na utafiti, ofisi, ufafiri, Tehama na
kadhalika.
Kuwajengea uwezo watumishi wake ili kuwa na
weledi wa kufanya utafiti kwa ufanisi.
Kubuni na kujenga uwezo wa kifedha ili
kuweza kuhudumia gharama za utafiti.
Kujenga na kutathmini mifumo bora na
endelevu ya kubaini mahitaji mbalimbali ya wafugaji na wadau wengineo
yanayohitaji majibu ya kitafiti.
Kujenga na kutathmini mifumo bora na
endelevu ya usambazaji wa matokeo ya utafiti kwa walengwa.
Kuongeza ufanisi wa usambazajji wa mifugo
bora, malisho na mbegu za malisho zilizokwishafanyiwa tafiti kwa wafugaji.
Taasisi hiyo inakusudia kujenga uwezo wa
vituo vyake, ikijumuisha kituo kikuu cha Mpwapwa, ili kuongeza uwezo na ufanisi
wa kufanya na kusambaza matokeo ya utafiti kwa walengwa.
Hata hivyo, MaendeleoVijijini
inatambua kwamba, bajeti ndogo ya Kilimo na Mifugo imekuwa ikileta changamoto
kubwa katika utekelezaji wa mikakati hiyo, hivyo ni vyema serikali ikawekeza
zaidi kwenye tafiti ili kuifanya sekta ya kilimo na mifugo isonge mbele.
Comments
Post a Comment