- Get link
- Other Apps
Featured Post
Posted by
Maendeleo Vijijini
on
- Get link
- Other Apps
Na Daniel Mbega, MaendeleoVijijini
FEBRUARI 23,
2017 msanii wa runinga Wema Isaack Sepetu aliamua kufanya kile ambacho wengi waliojeruhiwa
wamekuwa wakikifanya kwa hasira. Alijiunga na Chama cha Demokrasia na Maendeleo
(Chadema).
Wema,
ambaye ni Miss Tanzania wa mwaka 2006, alichukua uamuzi huo siku hiyo baada ya
‘kumsindikiza’ Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe, kwenye Mahakama Kuu
alikokwenda kuwasilisha kesi ya kikatiba Namba 1 ya mwaka 2017 akiitaka mahakama
hiyo itoe amri ya kuwazuia Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paulo Makonda,
Kamanda wa Polisi wa Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Simon Sirro, na Mkuu wa
Makachero wa kanda hiyo, ZCO Camillius Wambura, wasimkamate kwa tuhuma za
kujihusisha na dawa za kulevya.
Lakini
hata kabla ya kwenda mahakamani, tayari uamuzi wa Wema kujiunga na Chadema
ulikuwa umekwishafanyika, kwani ilielezwa mapema tu kwamba, baada ya
kuwasilishwa kwa kesi hiyo mahakamani, uongozi wa chama ungetangaza ama kuwakaribisha
wanachama wapya waliojiunga siku hiyo, akiwemo msanii huyo.
Uamuzi wa
Wema ‘kutafuta hifadhi ya kisiasa’ ndani ya Chadema ulifuatia kukamatwa kwake
na kushtakiwa yeye na wenzake wawili, mfanyakazi wake wa ndani Angelina Msigwa
(21) na mkulima Matrida Abas (16), baada ya kukutwa na kete ya bangi nyumbani
kwake katika operesheni kabambe iliyoanzishwa na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam,
Paulo Makonda.
Hata
alipokamatwa na kuwekwa mahabusu katika Kituo Kikuu cha Polisi Kati, Wema
aliona ‘ameonewa’ na akiwa mahabusu anadaiwa kuropoka maneno mengi akiilaani
serikali kwa nini imemkamata.
Baada ya
kusota mahabusu kwa siku kadhaa, hatimaye akafikishwa mbele ya Hakimu Mkazi wa
Mahakama ya Kisutu, Thomas Simba, kufanikiwa kupata dhamana wakati
akiwakilishwa na Wakili Msomi Albert Msando na wanatetewa na mawakili Albert
Msando na Nictagon Itege.
Haikushangaza
siku kesi yake ilipotajwa kwa mara ya pili Februari 22, 2017 kuona
akiwakilishwa pia na Mwanasheria Mkuu wa Chadema, Tundu Lissu, ambaye pia ni
Mbunge wa Singida Mashariki. Kesi hiyo itatajwa tena Jumatano hii Machi 15.
Wema
Sepetu, au yeyote yule, anayo haki ya kuchagua kuiunga na umoja ama chama
chochote kwa sababu ni haki yake ya Kikatiba.
Hata
hivyo, alichokifanya Wema pamoja na wengine ni uamuzi hasira ama kutaka kupata
hifadhi ya kisiasa kwa kuamini kwamba ‘wameonewa’ hata kama wamefanya makosa.
Wema,
inawezekana na wengine wote ‘wenye majina’, aliamini kwamba kwa umaarufu
alionao, basi ana kinga (immunity) ya kutokamatwa na yeyote, achilia mbali kuwekwa
mahabusu kwa siku kadhaa na kushtakiwa.
Msanii
huyo aliamini kwamba, kwa kuwa alikuwa mstari wa mbele kukiunga mkono chama
tawala, CCM, kiasi cha kugombea ubunge wa viti maalum huko mkoani kwao Singida,
ikiwa ni pamoja na kuzunguka na wasanii wenzake nchi nzima wakati wa kampeni za
uchaguzi mkuu mwaka 2015, basi hakuna ambaye anaweza kumgusa hata kama atakuwa
amefanya hatia.
Ndiyo
maana baada ya kujiunga na Chadema alikaririwa akisema kwamba, kama
asingejiunga na chama hicho alitamani kutoroka nchi akaishi kwingine, sijui
wapi!
Jambo
ambalo amelisahau ni kwamba, linapokuja suala la kisheria hakuna mtu ambaye
anaweza kuwa salama.
Kosa kubwa
ambalo amelifanya Wema na yeyote ambaye
ameamua kuvuka upande wa pili ni kuifanya operesheni ya dawa za kulevya kuwa ya
kisiasa, na mbaya zaidi Lissu naye ameamua kuvaa joho la utetezi siyo kwa
sababu ya kwamba Wema anayo haki hiyo tu, bali anataka kulifanya suala hilo
kama la kisiasa.
Wengi
wameunga mkono uamuzi wa Wema kukimbilia Chadema, wakisema kwamba huko ‘ndiko
nyumbani kwao’ na hakupaswa kuwa CCM.
Wanashindwa
kutambua kwamba, jinai haichagui mtu wala ni kikundi gani ambacho mtu huyo
amejiunga nacho, na zaidi wanaamini kwama operesheni ya dawa za kulevya
imechukuliwa kisiasa, jambo ambalo siyo kweli.
Wengine
wanaona Wema kujiunga na Chadema ni turufu kubwa kwa chama hicho kikuu cha
upinzani Tanzania Bara, kwamba anaweza kutumika kuushambulia upande wa pili na
wao wakajiongezea umaarufu kwa umaarufu wa msanii huyo.
Wema si
mwanaCCM peke yake aliyekumbwa na sakata hilo, kwani wapo wengi, wakiwemo
viongozi wa kuchaguliwa na wananchi ambao wamepata misukosuko hiyo kutokana na
kashfa za dawa za kulevya.
Diwani wa
Kata ya Mbagala Kuu, Yussuf Mehboob Manji, ni miongoni mwa washtakiwa kwa sasa
na alikaa mahabusu kwa siku sita mfululizo bila kuliona jua.
Vigogo
wengine wengi, wakiwemo makada wa CCM nao ni miongoni mwa watu walio kwenye
orodha ya watuhumiwa 65 wa dawa za kulevya.
Aidha,
wasanii wenzake kama ‘video queen’ Agnes Gerald ‘Masogange’, Naseeb Abdul
‘Diamond Platinumz’ ambaye walikuwa wote kwenye mzunguko wa kampeni za Chama
cha Mapinduzi, nao wamekwishafikishwa polisi na kuhojiwa.
Masogange
(28), ambaye naye alikaa mahabusu kwa siku nane, alikwishafikishwa katika
Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Februari 22, 2017 mbele ya Hakimu Mkazi Wilbard
Mashauri akikabiliwa na mashtaka mawili ya kutumia dawa za kulevya aina ya
heroin diacety na oxazepam. Kesi yake itatajwa tena Machi 21, 2017.
Ninachoweza
kusema ni kwamba, serikali huwa haikurupuki kufanya mambo yake kama baadhi ya
watu wanavyoaminishwa na wanasiasa, tena Jeshi la Polisi linatekeleza majukumu
yake kwa weledi mkubwa na kamwe maofisa wake hawawezi kwenda kumkamata mtu bila
hatia ama pasipo kujiridhisha.
Ni
masogange huyo huyo na mwenzake Melissa Edward (27) ambao Ijumaa ya Julai 5,
2013 walikamatwa kwenye uwanja wa ndege wa Oliver Tambo, Johannesburg nchini
Afrika Kusini wakiwa na shehena ya dawa za kulevya aina ya Crystal
Methamphetamine zenye thamani ya zaidi ya Shs. 6.8 bilioni wakitokea Tanzania.
Tukio hilo
lilitokea takriban wiki moja tu baada ya Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, Juni 28, 2013
kutangaza kuwa tatizo la dawa za kulenya ni janga la kitaifa.
Hata
hivyo, Masogange
na mwenzake waliachiliwa huru Septemba 19, 2013 na Mahakama ya Kempton ya
jijini Johannesburg, baada ya kulipa faini ya R30,000 (Sh4.8 milioni) kwa kosa
la kubeba kemikali zinazotumika kutengeneza dawa za kulevya.
Uamuzi wa
Wema kujiunga na Chadema kama ni wa kulazimishwa kutokana na mazingira yaliyopo
ya msako wa vigogo wa dawa za kulevya, basi unaweza kuwa ni mwanzo wa watu
wengi kukimbilia huko upinzani ikiwa wanaona serikali ya CCM inawaonea.
Binafsi
siwezi kushangaa kwa Chadema kuwapokea watuhumiwa wa aina yoyote, kwa sababu ni
kawaida yao kuifanya ‘haramu kuwa halali’.
Tumeshuhudia
namna viongozi wa chama hicho walipoyalamba matapishi yao kwa kuwazoa watu wote
ambao wao wenyewe waliwaita ni ‘mafisadi’, lakini wakawatakasa na kuona
‘malaika wa nuru’.
Tuliona
namna walivyomshawishi Edward Lowassa na hatimaye kumakabidhi mikoba ya
kugombea urais kupitia Chadema na hatimaye Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa),
ambayo awali alikuwa ameandaliwa Dk. Wilbrod Slaa, mara tu baada ya waziri mkuu
huyo wa zamani kuenguliwa katika kinyang’anyiro cha kuwania urais kupitia CCM.
Ni Lowassa
huyo huyo ambaye walimtuhumu kwa ufisadi na wakamwita majina mengi yasiyofaa,
lakini baadaye wakamtakasa na kumpamba kwa nyimbo na mapambio kwamba ndiye
‘rais wa mabadiliko’.
Kwa maana
hiyo, hata katika kadhia hii ya dawa za kulevya, wala sitashangaa kuona vigogo
wengi na makada wa CCM waliotajwa ama kuhusishwa wakikimbilia Chadema, chama
ambacho kinaleta tafsiri ya kupokea watuhumiwa wa aina zote na kuwaona wasafi.
Ni dhahiri
kwamba, kadhia hii ya dawa za kulevya imewajeruhi wengi, tena wale ambao
walikuwa wakionekana maarufu, wema na wakarimu mbele ya uso wa jamii.
Kwa maana
hiyo, ili kujitakasa kwamba ‘walionewa tu’ lazima watakimbilia mahali kupata
hifadhi. Huu ndio ukweli wenyewe.
0656331974
Comments
Post a Comment