- Get link
- Other Apps
Featured Post
Posted by
Maendeleo Vijijini
on
- Get link
- Other Apps
Alionekana kufurahia zaidi kuwa mwenyeji wangu, nikamwambia
nitakunywa Scotch. Akachukua chupa na glasi mbili kwenye saraka na kumimina
kiasi cha kutosha. Akaomba radhi kwa kutokuwa na barafu. Nikamwambia nimezowea
kugonga vitu vikali na hiyo haikuwa shida. Tulitaniana na tukagugumia vinywaji
vyetu. Ilikuwa ni Scotch nzuri sana.
“Ulichoniambia kuhusu Herman Jefferson kimenivutia sana,” nikamweleza.
“Nilikuwa nafikiria kama unaweza kunipatia taarifa zaidi. Ninajaribu tu
kupapasa. Jambo lolote linaweza kunisaidia.”
“Kwa nini, hakika nitakupa.” Alinitazama kwa namna mbwa wa
Mchungaji anaweza kuonekana mara anaposikia sauti ya fadhaa. “Ulikuwa na
mtazamo gani mawazoni mwako?”
Nikampa mtazamo wangu wa mshangao wa kama-ningejua ambao huutumia
ninapokutana na watu wa aina ya Jay Wayde.
“Sielewi,” nikamwambia. “Kazi yangu ni kukusanya taarifa sahihi
kwa kadiri yoyote kwa matumaini ya kwamba zinaweza kuleta maana. Kwa mfano,
kama ulimfahamu Jefferson. Uliniambia jambo fulani kuhusu tabia yake. Uliniambia
alikuwa na fujo, mlevi kidogo, alianzisha ugomvi na kusababisha fujo. Alikuwaje
wakati alipokuwa na wanawake?”
Uso wa Wayde ghafla ulionyesha matumaini.
Nilifikiri jinsi alivyokuwa katika suala la wanawake. Hisia zake
za mapenzi zingeweza kuzuiwa na rungu la kuchezea golfu.
“Alikuwa anapenda mno wanawake. Sawa, unapokuwa kijana, unaweza
kutembea na wasichana — Mimi pia nilikuwa na wasichana, lakini Herman alikuwa
ameoza. Kama baba yake asingekuwa na uwezo mkubwa katika jiji hili, kungekuwa
na skendo kila siku kumhusu yeye.”
“Kulikuwa na msichana yeyote maalum?” nikamuuliza.
Alisita, kisha akasema, “Sipendi kutaja majina, lakini kulikuwa na
huyu msichana, Janet West. Ni katibu muhtasi wa Bwana Jefferson. Ali . . .” Alisita
ghafla na macho yake yakaangalia pembeni. “Tazama, samahani, sidhani kama ni sahihi
kuzungumzia hili. Hata hivyo, hili lilitokea takriban miaka tisa iliyopita. Najua
kwa sababu Herman aliniambia, lakini hilo halinipi haki ya kukueleza.”
Niliona kwamba alikuwa anapenda sana kunieleza: akipenda kushiriki
katika kumsaka muuaji na akijiona ni mtu muhimu sana kiasi kwamba mimi nilikuwa
na nia ya kusikia kile atakachoniambia.
Hivyo nikamwambia kiujanja, “Kila kipande cha taarifa
nitakachopata kinaweza kuniongoza kwa muuaji. Unaweza kujiuliza mwenyewe kama
una haki ya kunieleza ama kutonieleza.”
Hili lilimfurahisha sana. Macho yake yakarejewa na nuru na
kuinamia mbele, akinitazama usoni.
“Sawa, ni vyema, kwa kuliweka namna hiyo, ninajua unachomaanisha.”
Alipapasa nywele zake zilizokatwa vyema na kisha kuonyesha mtazamo wa mtu
ambaye hana rekodi za skendo, akasema, “Herman na Janet West walikuwa na
uhusiano wa mapenzi takriban miaka tisa iliyopita. Walipata mtoto. Herman akamkataa na Jane West
akamwendea baba yake ambaye alifadhaika sana. Bahati mbaya mtoto alikufa. Yule mzee
alisisitiza Herman amuoe binti huyo, lakini Herman akakataa kata kata. Nadhani yule
mzee akaamua mwenyewe kumchukua jumla. Akampeleka nyumbani kwake na kumfanya
kuwa katibu muhtasi wake. Herman aliniambia kuhusu hili. Alikuwa amekasirika
kuona baba yake amemchukua binti huyo na kumpeleka nyumbani kwake. Nahisi mzee
alitarajia Herman angeweza kubadili moyo wake na kumuoa, lakini wakati
matumaini yalipokufa na kubaini kwamba Herman asingeweza kubadili uamuzi wake, akaamua
kufanya mipango ya Herman kwenda Mashariki. Janet amekuwa na mzee tangu wakati
huo.”
“Ni mzuri sana,” nikamwambia. “Sielewi kwa nini hajaolewa mpaka
sasa.”
“Hainishangazi kabisa. Yule mzee asingependa. Anamtegemea sana yule
binti, na zaidi ya yote, hakuna mtu mwingine yeyote atakayemwachia urithi wake
wa mamilioni baada ya Herman kufariki.”
“Hakuna yeyote?” Nikajaribu kuficha hamu yangu ya kusikia
kipengele hicho. “Anaweza kuwa na ndugu.”
“Hapana. Nilikuwa naifahamu familia ile vizuri sana. Herman aliniambia
kwamba ndiye angerithi kwa sababu hakukuwepo na watu wengine. Nina uhakika
Janet anaweza kupata urithi, hata sehemu yake tu, mara mzee atakapofariki.”
“Ni bahati yake, mke wa Herman hawezi kuidai.”
Akaonyesha kugutuka.
“Sikuwahi kufikiria kuhusu upande huo. Hana nafasi kubwa. Sidhani kama
yule mzee angeweza kumwachia mwanamke wa Kichina chochote.”
“Kama mke halali wa Herman, angeweza kufungua madai. Kama jaji
atakuwa na huruma, angeweza kuchukua urithi.”
Mlango wa upande wa kulia ukafunguliwa na msichana akaingia akiwa na rundo la barua zilizohitaji
kusainiwa. Alikuwa ni aina ya wasichana ambao nilitarajia Wayde angewaajiri: mrembo,
na mwenye miwani.
Nikasimama wakati alipoweka barua hizo mezani.
“Ngoja niende,” nikasema. “Tutaonana tena.”
“Kuna maendeleo yoyote?” aliuliza baada ya yule binti kuondoka. “Polisi
wamegundua chochote?”
“Hakuna chochote walichogundua. Uchunguzi rasmi wa kisheria
utafanyika kesho, lakini watalazimika kuleta mashtaka ya mauaji yanayowahusu
watu wasiojulikana. Yalikuwa ni mauaji yaliyotumia akili nyingi sana.”
“Nitakwambia.” Akavuta barua mbele yake. “Kama kuna lolote
nitakaloweza kulifanya. . .”
“Nitakueleza.”
Niliporudi ofisini kwangu, nikampigia Retnick na kumweleza nini
nilichokipata kumhusu Janet West.
“Mpira sasa uko miguuni mwako,” Nikamwambia. “Kama ningekuwa wewe,
ningependa kujua ni wapi alikokuwa Bi West majira ya saa tisa alfajiri wakati
mwanamke wa Kichina alipouawa.”
Kulikuwa na utulivu wakati nikisikiliza jinsi alivyokuwa akipumua
kwa nguvu.
“Lakini sasa wewe siyo mimi,” hatimaye akajibu. “Tutaonana katika
uchunguzi. Usisahau kuvaa shati zuri. Ofisa mchunguzi wa vifo ni mwanaharamu,” na
akakata simu.
Itaendelea kesho...
Comments
Post a Comment