- Get link
- Other Apps
Featured Post
Posted by
Maendeleo Vijijini
on
- Get link
- Other Apps
Mkurugenzi wa MSD, Laurean Bwanakunu, akizungumza na wanahabari jijini Dar es Salaam hivi karibuni kuhusu kuimarika kwa upatikanaji wa dawa.
Na Daniel Mbega, Dar es Salaam
SERIKALI imeendelea kuwachezesha shere Watanzania kuhusu suala la
upatikanaji wa dawa na vifaa tiba katika vituo vya afya kwa kurudia taarifa
zile zile ambazo zimekuwa zikilalamikiwa, FikraPevu inaandika.
Katika kipindi cha takriban miezi mitatu, serikali imetoa kauli kadhaa
zinazotofautiana na uhalisia, huku ikiendelea kukanusha taarifa za uhaba wa
dawa na vifaa tiba wakati ambapo ukweli halisi unaonyesha kuna tatizo.
Kwa mujibu wa uchunguzi wa FikraPevu, kauli mbili zilizotolewa na Wizara pamoja na Bohari ya Madawa (MSD)
kwamba upatikanaji wa dawa umeimarika haziakisi uhalisia wa tatizo ambalo
linaonekana kuwa bomu linalosubiri muda kulipuka.
Ijumaa, Januari 6, 2017, Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Maendeleo
ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dk. Mpoki Ulisubisya, alikaririwa akirudia
kauli zililizozoeleka tangu wakati wa Bunge la Bajeti, kwamba jumla ya Shs. 251
bilioni zimetengwa ili kuimarisha upatikanaji wa dawa katika vituo vya afya na
zahanati zote nchini.
Kauli hiyo ambayo aliitoa wakati wa kipindi cha ‘Timatekeleza’
kinachorushwa na runinga ya taifa, TBC1, inaelezwa kwamba ni ya kisiasa zaidi,
kwani kiasi cha fedha kinachotajwa siyo tu kwamba hakitoshi, bali karibu nusu
yake kinapaswa kulipia deni la Shs. 108 bilioni ambalo serikali ilikuwa
inadaiwa na MSD kabla hata ya Bajeti ya mwaka 2016/17.
Aidha, uchunguzi wa FikraPevu unaonyesha kwamba, kiasi cha Shs. 251 bilioni ni pungufu kwa takriban
47% kutoka mahitaji halifi ya dawa nchini ambayo ni Shs. 577 bilioni kwa mwaka.
Mtendaji huyo wa serikali alisema kupitia runinga kwamba taarifa
za upungufu wa dawa nchini zinapaswa kupuuzwa kwa kuwa bajeti ya mwaka huu wa
fedha ni kubwa na inaweza kukidhi mahitaji ya dawa.
“Taarifa zinazozagaa juu ya upungufu wa dawa katika zahanati hapa
nchini si za kweli, napenda kuwatoa hofu wananchi na bajeti yetu ya mwaka huu
ni Shs. 251 bilioni kwa ajili ya dawa tu,” alisema Dk. Ulisubisya.
Dk.
Ulisubisya alisisitiza kuwa kufikia mwezi Mei 2017 asilimia 90 ya dawa zote
zitakuwa zimepatikana na kusambazwa kwenye vituo vya afya na zahanati zote
nchini ili kuimarisha sekta ya afya na kwamba mpaka sasa chanjo zote zipo za
kutosha.
“Tunataka
kila kituo cha afya kinachojengwa sasa hivi kitoe huduma za upasuaji ili
kupunguza mlundikano wa wagonjwa wanahoitaji huduma hiyo na kuokoa maisha
ya mtanzania kwa haraka zaidi,” alisema Dk. Ulisubisya.
Katika kuendelea kuwafanya Watanzania waishi kwa matumaini, siku
nne baadaye, yaani Jumanne, Januari 10, 2017, Mkurugenzi wa MSD, Laurean Bwanakunu, akizungumza na wanahabari
katika Ukumbi wa Idara ya Habari – Maelezo jijini Dar es Salaam, alisema hali
ya upatikanaji wa dawa imeboreshwa kutoka asilimia 54 iliyokuwepo mwaka 206
hadi kufikia asilimia 74 hivi sasa.
Mkurugenzi huyo wa MSD
aliwahakikishia Watanzania kwamba upatikanaji wa dawa utaimarika mwishoni mwa
mwezi Machi 2017 hadi kufikia asilimia 90, tofauti na kauli ya Dk. Ulisubisya
aliyesema kiwango hicho kitafikiwa Mei 2017.
“Kwa sasa aina za dawa
muhimu 100 kati ya 135 zinazohitajika kuwepo MSD zinapatikana kwenye maghala ya
MSD kote nchini,” alisema.
Itakumbukwa kwamba,
Septemba 2016, taasisi isiyo ya kiserikali ya Sikika, ilisema kwamba kulikuwa
na upungufu mkubwa wa dawa na vifaa tiba nchini kama ilivyokuwa imeripotiwa na
vyombo vya habari vya ndani na nje, hususan kituo ch runinga cha Al-Jazeera,
lakini Septemba 27, 2016 serikali ikakanusha kwa herufi kubwa kwamba taarifa
hizo zilikuwa za uongo.
Hata hivyo, vyombo vya habari vilikuwa vimenukuu takwimu katika
tovuti rasmi ya MSD kwamba kulikuwa na upungufu wa asilimia 47 ya aina
mbalimbali za dawa zilizotakiwa kuwepo kwenye orodha ya dawa MSD.
Wakati upungufu huo ukiripotiwa, serikali, ikiwemo MSD yenyewe,
ilikanusha kwa kusema aina ya dawa zilizokuwepo ni asilimia 53, bila kueleza
ukweli kuwa kulikuwa na uhaba wa asilimia 47 ya aina nyingine ambazo zilipaswa
kuwepo.
Sikika ilihoji uhalali wa kanusho la serikali kwamba taarifa
zilizoripotiwa zilikuwa za uongo kwa kusisitiza kwamba, mtu akisema uhaba ni
asilimia 47 ya aina ya dawa na mwingine akasema uwepo ni asilimia 53 wote
wanamaanisha kitu kile kile.
“Badala ya kujibu hoja ya msingi, yaani upungufu wa dawa nchini
kwa ujumla; Wizara iliamua kujikita kwenye kutaja uwepo wa baadhi ya dawa kama
vidonge vya paracetamol na zingine chache.
“Bohari Kuu ya Dawa ilinukuliwa na vyombo vya habari ikikanusha
uwepo wa upungufu wa dawa na kusema serikali imefanya maajabu kwa kuipatia MSD
jumla ya Shs. 20 bilioni kwa robo ya 2016/2017.
“Hata hivyo, bilioni 20 ni pungufu ya kiwango halisi ambacho
kingehitajika (Shilingi bilioni 62.5), kwa robo ya kwanza ya mwaka iwapo bajeti
iliyotengwa ya shilingi bilioni 251 ingegawanya sawa na kutolewa katika awamu
nne. Je, Bohari Kuu ya Dawa inaposema serikali imefanya maajabu ina maana
haihitaji fedha zaidi kwa ajili ya kutatua tatizo la dawa nchini?” ilihoji
taarifa ya Sikika.
Sikika ilieleza katika taarifa yake kwamba, uhaba wa dawa na vifaa
tiba katika Bohari Kuu ya Dawa siyo tatizo jipya, bali ni la muda mrefu, ambalo
serikali yenyewe imekuwa ikikiri kupitia taarifa zake mbali mbali, na kwamba
sasa limefikia kiwango kikubwa hata kupelekea uhaba wa dawa kama za chanjo kwa
kipindi cha zaidi ya miezi mitatu.
Aidha, shirika hilo lilisema kwamba, Wizara ya Afya imekuwa ikiahidi
bungeni kila mwaka kulipa deni inalodaiwa na MSD ili kuboresha ufanisi wa
bohari, lakini uhaba wa dawa umeendelea kuwepo na deni la MSD limekuwa likikua
kila mwaka.
Kukosekana kwa dawa na vifaa tiba kunakwamisha kasi ya serikali
kutekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo kuelekea mwaka 2025 kuhusu suala la afya,
lakini inashindwa kutekeleza kwa ukamilifu lengo namba 3 kati ya malengo 17 ya
Malengo Endelevu ya Dunia (SDG) kama yalivyopitishwa na Umoja wa Mataifa
Septemba 22, 2015.
Oktoba 10, 2016, Waziri wa Afya, Ummy
Mwalimu, aliwaeleza wanahabari kwamba, taarifa za upungufu wa dawa katika
Bohari Kuu ya Dawa hazikuwa za kweli na kwamba hali ya upatikanaji wa dawa
ilikuwa vizuri ambapo zilikuwepo dawa za antibiotics muhimu kama Amoxycillin,
Ciprofloxacin, Cotrimoxazole na Doxycycline na dawa za maumivu kama
Paracetamol, Asprin na Diclofenac zilikuwepo za kutosha.
Akaongeza kwamba, dawa za Kifua Kikuu,
Ukoma na zile za kufubaza makali ya Ukimwi (ARVs) nazo zilikuwepo.
Lakini akakiri kwamba, chanjo za
watoto na wajawazito kweli jazikuwepo kwa miezi miwili, lakini kwa wakati huo
zilikuwa zinapatikana.
Waziri Mwalimu alikwenda mbali zaidi
kwa kusema kwamba, serikali ilikuwa imetenga Shs. 85 kulipa deni la MSD.
Siku tatu baada ya kauli ya Waziri Ummy Mwalimu, Makamu wa Rais,
Mhe. Samia Suluhu Hassan, wakati wa uwekaji wa jiwe la msingi la jengo la wodi
ya wazazi kwenye Hospitali ya Mwananyamala, alikiri kuwapo uhaba wa dawa na
vifaa tiba katika hospitali za Serikali nchini.
Akasema uhaba wa dawa ni changamoto ya muda mfupi kwani Serikali
inatafuta ufumbuzi wa haraka kuwahudumia wananchi.
“Tumetenga Shs. 70 bilioni kwa ajili ya kumaliza tatizo la dawa
nchini, pia tumetenga jumla ya Shs. 85 bilioni kwa ajili ya kupunguza deni MSD.
Nia yetu ni kutaka huduma za afya ziwe zenye ubora,’’ alisema.
Aidha, katika kile kinachoonekana mkanganyiko mkubwa
kwa wananchi, Desemba 2, 2016, akiwa ziarani mkoani Arusha, Waziri Mkuu
Majaliwa Kassim Majaliwa, alikaririwa akisema kwamba serikali imetoa Shs. 1
trilioni kwa ajili ya ununuzi wa dawa za aina mbalimbali ili kuondoa upungufu
wa dawa kwenye hospitali nchini.
“Awali tulitoa Shs. 40 bilioni kwa ajili ya dawa na
sasa tumeongeza fedha hadi kufikia shilingi trilioni moja,” alisema Waziri Mkuu
wakati akizungumza na watumishi wa idara na taasisi mbalimbali za serikali
wakiwemo watumishi wa Halmashauri ya Jiji la Arusha na Wilaya ya Arusha.
Hata hivyo, fedha zinazotajwa na Waziri Mkuu kwamba ni Shs. 1
trilioni kwa ajili ya ununuzi wa dawa hazijulikani zimetoka katika fungu gani,
kwa sababu bajeti ya Wizara ya Afya kwa mwaka 2016/17 ni Shs. 845,112,920,056 kama
ilivyopitishwa Mei 11, 2016.
Kati ya hizo, Shs. 317,752,653,000 kati ya hizo zilikuwa za
matumizi ya kawaida na Shs. 527,360,267,056 kwa ajili ya utekelezaji wa miradi
ya maendeleo, ambayo ni pamoja na ununuzi wa dawa na vifaa tiba.
Aidha, inafahamika kwamba, siyo fedha zote zinazoidhinishwa ambazo
hutolewa na mfano halisi ni kwa bajeti ya mwaka 2015/16 ambapo ziliidhinishwa
Shs. 780,740,723,000, na Shs. 340,098,271,000 zilikuwa kwa matumizi ya kawaida
na Shs. 440,642,452,000 za miradi ya maendeleo.
Lakini zilizopokelewa hadi kufikia mwezi Aprili zilikuwa Shs.
604,547,066,537 ambazo ni asilimia 77.4 tu ya kiasi kilichoidhinishwa na Bunge.
Kati ya fedha hizo, Shs. 269,205,005,123 zilikuwa za matumizi ya kawaida na
Shs. 335,342,061,414 ni fedha za miradi ya maendeleo.
Suala la ununuaji wa dawa limekuwa na changamoto kubwa kwa miaka
mingi sasa kwani bajeti inayotengwa haikidhi mahitaji, jambo ambalo siyo tu
linasababisha upungufu wa dawa na vifaa tiba, bali linaendelea kupandisha deni
la serikali kwa MSD.
Bajeti zinazotengwa kwa ajili ya
kununulia dawa na vifaa tiba imekuwa ikiongezeka kwa asilimia kidogo ambapo kwa
miaka sita iliyopita takwimu zinaonyesha kwamba mwaka 2011/2012 bajeti iliyotengwa
ilikuwa Shs. 23.7 bilioni.
Kwa mwaka 2012/2013 bajeti ilikuwa
Shs. 34 bilioni, mwaka 2013/2014 ilikuwa Shs. 34 bilioni, mwaka 2014/2015
ilikuwa Shs. 60 bilioni, lakini mwaka 2015/2016 ikashuka hadi Shs. 30 bilioni
kabla ya kuongezwa mwaka 2016/17 na kufikia Shs. 251.5 bilioni.
Ingawa kutokana na mwenendo wa serikali ya sasa watendaji
wanaogopa kuzungumzia jambo lolote kwa hofu ya ‘kutumbuliwa’, lakini uhalisia
ni kwamba tatizo la uhaba wa dawa ni sugu na inaonekana kauli nyingi za
serikali zina mlengo wa kisiasa zaidi.
Uchunguzi wa Fikra Pevu
unaonyesha kwamba takriban asilimia 80 ya wananchi hawamo katika mfumo wowote
wa bima za afya, na inapotokea uhaba wa dawa na vifaa tiba, hujikuta
wakiathirika zaidi kwani hulazimika kutumia gharama kubwa kupata huduma, na
wakati mwingine hukosa kabisa.
MSD imekuwa ikiripotiwa kwamba inashindwa kutoagiza dawa kama njia
ya kulinda mtaji wake ambao umekuwa ukizidi kutetereka kutokana na madeni
yanayozidi kulimbikizwa serikalini pamoja na vituo vya kutolea huduma.
Inaelezwa kwamba, Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii pekee inadaiwa
na MSD zaidi ya Shs. 90 bilioni, wakati Muhimbili inadaiwa Shs. 8 bilioni.
CHANZO: FIKRAPEVU
Comments
Post a Comment