- Get link
- Other Apps
Featured Post
Posted by
Maendeleo Vijijini
on
- Get link
- Other Apps
ZILIKUWA ni dola mia
tatu rahisi zaidi ambazo Nelson Ryan ameweza kuzipata, lakini ghafla akagundua
kwamba alikuwa amejiingiza mtegoni. Mwito wa simu, ukionekana hauna kasoro
yoyote, ulimwongoza kwenye mauaji ya binti wa Kichina aliyepiga simu huku
akiongea sana. Simu hiyo pia ikamwongoza moja kwa moja kwenye maisha ya
kihalifu ya Hong Kong. Tangu sasa na kuendelea, Ryan hakuweza kufanya chochote mpaka
atakapompata muuaji ambaye amemwingiza kwenye majanga. ENDELEA…
“Unadhani unakwenda wapi?” akahoji.
“Ofisini kwangu,” nikamwambia. “Hilo
linakutisha?”
“Luteni atakapokuwa tayari kukuona,
nitakwambia. Nenda kaketi kwenye mojawapo ya magari yale.”
Nikaenda kwenye mojawapo ya magari
ya polisi na kuketi kwenye viti vya nyuma. Umati wa watu arobaini uliokuwa
umekusanyika, ukageuka kunitazama mimi badala ya ambulance. Nikawasha sigara na
kujaribu kuwapuuza.
Nikaketi pale nikivuta sigara na
kuiacha akili yangu kufanya kazi kwa yaliyopita na yaliyopo bila kuiruhusu
ifikirie yajayo. Kwa kadiri nilivyoifikiria hatma yangu ndivyo nilivyozidi
kuchukia. Nilikuwa nahisi kwamba niko mtegoni.
Baada ya takriban saa moja wauguzi
wawili wakatoka wakiwa wamebeba machela. Binti wa Kichina, chini ya shuka,
alionekana mdogo kama mtoto. Umati ukapiga kelele za kawaida zinazotolewa na
umati wakati hatari inapotokea. Wauguzi wakauweka mwili kwenye ambulance na
kuondoka. Dakika chache baadaye Ofisa Afya akatoka, akaingia kwenye gari lake
na kuongozana na ambulance.
Nikasubiri kwa muda mrefu, halafu
polisi wa alama wakatoka. Mmoja wao akamuonyesha ishara polisi aliyekuwa
akinilinda. Wote wakaingia kwenye magari yao na kuondoka.
Polisi huyo akafungua mlango na
kuniashiria nitokea.
“Haya twende,” akasema. “Luteni
anakuhitaji.”
Wakati nilipopita kwenye kiambaza,
Jay Wayde, Mkemia wa Viwanda, ambaye alikuwa na ofisi jirani na mimi akatoka
kwenye gari lake. Akaungana nami kwenye lifti.
Nilikuwa nimemzidi miaka mitatu au
minne: mtu mwenye umbile kubwa, la kimazoezi akiwa amenyoa denge, uso mpana na
macho maangavu. Mara kwa mara tulikutana na kupanda wote lifti kwenda kwenye
gari zetu. Alikuwa jamaa wa kawaida na kama alivyo Sparrow, alikuwa amevutiwa
na namna ya maisha yangu. Nadhani watu wengi wenye heshima zao hawawezi
wakasita kuvutiwa na maisha ya wanaoitwa wapelelezi. Kila wakati alipenda
kuniuliza mambo ya kuvutia niliyoyapitia, na kwa muda mfupi tuliokuwa kwenye
lifti na kuelekea kwenye magri yetu, nilimweleza uongo kama niliomwambia Sparrow.
“Nini kinaendelea?” aliuliza wakati
lifti ikipanda kuelekea ghorofa ya nne.
“Nimemkuta binti wa Kichina akiwa
amefia ofisini kwangu asubuhi hii,” nikamwambia. “Polisi wamevutiwa na tukio
hili.”
Alinitazama.
“Amekufa?”
“Kuna mtu alimuua.”
Taarifa hii fupi ilionekana
kumchanganya.
“Unamaanisha ameuawa?”
“Ndilo neno la kiufundi.”
“Oooh! Kwa jina la Mike!”
“Nimekuwa nikisema vivyo hivyo tangu
nilipomkuta.”
“Nani aliyemuua?”
“Ah! Sasa hilo ndilo swali. Wewe
jana uliondoka saa ngapi? Ulikuwepo ofisini wakati ninaondoka.”
“Majira ya saa tatu. Mlinzi alikuwa
anafunga.”
“Hukusikia mlio wa bastola?”
“Kwa Jina la Mungu . . . hapana!”
“Wakati unaoondoka uliona mwanga
wowote kwenye ofisi yangu?”
“Hakukuwepo na mwanga. Hivi siyo
nilikusikia ukiondoka majira ya saa kumi na mbili?”
“Ni kweli kabisa.”
Nikachanganyikiwa sasa. Binti huyu
wa Kichina atakuwa ameuawa baada ya saa tatu usiku. Ushahidi wangu ulionekana
kuwa mgumu kuliko kuku aliyenyeshewa.
Lifti ikasimama kwenye ghorofa ya
nne. Tukatoka nje. Mlinzi na Sajini Pulski wakatoka ofisini kwangu. Mlinzi
alinitazama kana kwamba nilikuwa zimwi la vichwa viwili. Wakaingia kwenye lifti
na kushuka chini.
“Nadhani utakuwa na hekaheka,” Wayde
alisema, akimtazama polisi aliyesimama kwenye mlango wa ofisi yangu. “Kama kuna
lolote ninaloweza kufanya . . .”
“Asante,” nikamwambia. “Nitakutaarifu.”
Baada ya kuachana naye, nikampita
polisi na kuingia kwenye ofisi ya nje. Zaidi ya njiti za vibiriti na vipisi vya
sigara vilivyotapakaa kwenye vikasha maalum, chumba kilikuwa na mwonekano wa
utupu. Nikaingia kwenye ofisi yangu ya ndani.
Luteni Retnick alikuwa ameketi nyuma
ya dawati langu. Alinitazama kwa jicho la kipolisi wakati nikiingia, na
akaniashiria niketi kwenye kiti cha wageni.
Kulikuwa na harufu ya damu kavu
nyuma ya kiti. Sikutaka kuigusa hivyo nikaketi kwenye mkono wa kiti. “Una
leseni ya kumiliki bunduki?” akauliza.
“Ndiyo.”
“Bunduki yako aina gani?”
“.38 police special.”
Akaweka kiganja chake mezani.
“Nipe.”
“Iko kwenye saraka ya juu ya meza
upande wa kulia.”
Akanitazama kwa muda mrefu, halafu
akaondoa mkono wake.
“Haipo. Nimechunguza kwenye meza
yako yote.”
Nilijizuia kufuta kijasho chembamba
kilichoanza kuchuruzika kwenye shingo yangu.
“Hapo ndipo ninapoiweka.”
Akachukua sigara kubwa kutoka kwenye
boksi lake, akaikunjua karatasi, akaikata kidogo, na kuiweka mdomoni baada ya
kuiwasha. Muda wote macho yake yalikuwa yakinitazama.
“Ameuawa na .38,” alisema. “Ofisa wa
Afya anasema amekufa majira ya saa tisa alfajiri. Tazama, Ryan, kwa nini
usiseme tu? Kwani huyu mwanamke alikuwa na nini kwenye mkoba wake?”
Nikiidhibiti sauti yangu kwa juhudi
kubwa, nikamwambia, “Ninaweza kuonekana kwako kama bwege, mpumbavu, lakini
huwezi kuamini kwamba nitakuwa mpumbavu kiasi hicho cha kumuua ofisini kwangu
na nikitumia bunduki yangu hata kama angekuwa na dhahabu zote za Fort Knox kwenye
mkoba wake.”
Akawasha sigara yake na kupuliza
moshi wote kwangu.
Itaendelea
kesho…
Comments
Post a Comment