- Get link
- Other Apps
Featured Post
Posted by
Maendeleo Vijijini
on
- Get link
- Other Apps
“Kama tusipokuwa makini, huyu
mwendawazimu atatuibia kazi zetu.”
Pulski alitoa kitu fulani kwenye
gego lake na kukitema kwenye zuria langu. Hakusema chochote: haikuwa kazi yake
kuzungumza. Alikuwa msikilizaji mzuri.
Retnick akatafakari kwa muda. Ilikuwa
ni namna iliyompa maumivu kiasi. Hatimaye, akasema, “Nitakwambia kwa nini
unafikiri upuuzi huo, kijana mjanja. Huyu bwana alikupigia simu kutoka uwanja
wa ndege ambao ni maili mbili kutoka hapa. Kama hudanganyi, uliondoka ofisini
kwako baada ya saa kumi na mbili. Asingeweza kufika hapa mapema kabla ya saa
moja na nusu kutokana na foleni ya magari kwenye barabara kuu kwa wakati huo,
na kwa yeyote, hata kwa mwenye ngozi ya manjano, atatambua kwamba huo ni muda
baada ya saa za kazi. Binti huyu asingekuja hapa kwa kubahatisha kwamba
angekukuta. Angeweza kukupigia simu kwanza.”
“Nini kinachokupa uhakika kwamba
hakupiga simu? Pengine alipiga na Hardwick
alikuwa ofisini kwangu kuipokea. Pengine alimwambia atamsubirina kwamba yeye
aje moja kwa moja.”
Kwa kubadilika kwa uso wake nikajua
alikuwa anejilaumu mwenyewe kwa kushindwa kufikiria hivyo kwanza.
Ofisa wa afya, na wafanyakazi
wawili, wakiwa na machela waliwasili mlangoni.
Pulski akajilazimisha kupisha
mlangonina kumuongoza Ofisa wa Afya, mtu mfupi na uso ulioshupaa, hadi kwenye
chumba cha ndani kuitazama maiti.
Retnick akarekebisha tai yake.
“Isingekuwa vigumu kumpata binti
huyu,” alisema kana kwamba alikuwa akizungumza peke yake. “Wakati mtu mwneye
ngozi ya manjano ni mrembo kama huyu, anafahamika mara moja. Umesema lini tena
huyu bwana Hardwick angekupigia simu?”
“Kesho —Ijumaa.”
“Unadhani atapiga?”
“Haiwezekani.”
Akatikisa kichwa kukubali.
“Yeah.” Akaitazama saa yake, halafu
akapiga mwayo. “Unaonekana kama kituko. Unaonaje kama ukienda kupata kikombe
cha chai? Usiende mbali na usifungue mdomo wako. Nitakuwa tayari kuzungumza na
wewe baada ya nusu saa.”
Kwa muda sikuwa najidanganya. Hakuwa
anafikiri ama kukubali mawazo yangu: alitaka nikae pembeni.
“Nadhani ninaweza kupata kahawa,” nilisema.
“Ninaweza kwenda nyumbani walau kuoga?”
“Nani anayejali kama unanuka jasho?”
akajibu. “Kunywa kahawa na ukae mahali ambako unaweza kuonekana.”
Nilishuka kwenye lifti. Japokuwa
ilikuwa saa mbili na dakika ishirini, umai mdogo ulikuwa umekusanyika kuangalia
ambulance iliyokuwa inasubiri na magari manne ya polisi yaliyoegeshwa mbele ya
jengo. Wakati nikielekea pale Quick Snack Bar nikasikia vishindo nyuma yangu.
Sikujisumbua kugeuka. Nilitegemea kunywa kahawa chini ya ulinzi wa polisi.
Niliingia kwenye baa na kuketi
kwenye stuli. Sparrow, macho yakiwa yamemtoka pima, akaondoka dirishani
alikokuwa akiangalia ambulance na kunitazama kwa shauku.
“Nini kinachoendelea, Bwana Ryan?” akauliza,
pumzi akiwa amezibana.
“Kahawa, chungu na nyeusi na ufanye
haraka,” nikamjibu, “halafu mayai mawili ya kukaanga na mkate.”
Polisi aliyevaa kiraia ambaye
alinifuata hakuingia kwenye baa. Alisimama nje ambako angeweza kuniona vizuri.
Akizuia shauku yake kwa nguvu
zilizofanya michirizi myeusi kwenye kwapa zake, Sparrow alimimina kahawa na
kuanza kukaanga mayai.
“Kuna mtu amekufa, Bwana Ryan?” aliuliza
wakati akivunja mayai na kuyaweka kwenye kikaango.
“Unafunga muda gani usiku?” nikamuuliza,
huku nikimtazama polisi aliye nje ambaye alinitisha kupitia kwenye kioo cha
dirisha.
“Saa nne kamili,” Sparrow akasema, akijaribu
kuonyesha umakini bila mafanikio. “Nini kinachoendelea pale?”
“Mwanamke wa Kichina ameuawa.” Nilikunywa
kahawa kidogo. Ilikuwa ya moto na chungu na nzuri. “Nimemkuta ndani ya ofisi
yangu saa moja iliyopita.”
Koo lake likapanda na kushuka ghafla.
“Usinitanie, Bwana Ryan?”
“Ukweli wa Injili.” Nilimaliza
kahawa na kumsogezea kikombe. “Ongeza nyingine.”
“Mwanamke wa Kichina?”
“Yeah. Usiulize maswali. Najua zaidi
kama unavyojua wewe. Ulimuona mwanamke wa Kichina akienda kwenye jengo ilipo
ofisi yangu mara baada ya mimi kuondoka?”
Akatikisa kichwa chake wakati
akijaza kahawa nyingine kwenye kikombe.
“Hapana. Nadhani ningemuona kama
angekwenda kabla sijafunga baa. Sikuwa na kazi nyingi jana usiku.”
Nikaanza kutokwa jasho taratibu.
Nilikuwa na ushahidi hadi saa mbili na nusu: muda ambao msichana na yule
mwanamume mkimbiaji waliponipita kule mlimani nikiwa nimeegesha gari. Ninadhani
wakati huo mwanamke wa Kichina tayari alikuwa ofisini kwangu wakati huo. Baada
ya saa mbili na nusu, ilikuwa ni juu yangu mimi kusema nilikuwa nimeketi usiku
kucha nje ya jumba tupu la Jack S. Myers Jr..
“Hukumuona mgeni yeyote akienda pale
baada ya mimi kuondoka hadi wakati ulipofunga?”
“Siwezi kusema nilimuona. Majira ya
saa tatu mlinzi wa pale alifunga kama kawaida.” Alinipatia mkate na mayai. “Nani
aliyemuua?”
“Sijui.” Ghafla nikawa nimepoteza
hamu ya kula. Mtego huu sasa ukaanza kuonekana mbaya kwangu. Nilimjua Retnick. Alikuwa
mtu ambaye alipenda kushikilia jambo. Kama sikuwa na ushahidi wa kutosha ambao
ungemshawishi mtu mpumbavu, lazima angenibana. “Unaweza kuwa hukumuona, au siyo?”
“Nadhani hiyo ni sahihi. Sikuwa
natazama nje ya dirisha muda wote.”
Wanaume wawili wakaingia na kuagiza
chamsha kinywa. Wakamuuliza Sparrow nini kilichokuwa kinaendelea. Baada ya
kunitazama, akawaambia hajui. Mmoja wa watu hao, mnene aliyevaa jaketi la ngozi
aina ya Brando akasema, “Mtu ameuawa. Angalia gari lile pale nje.”
Nikaisogeza pembeni sahani yangu.
Sikuwa na uwezo wa kula chakula wakati huu. nilimalizia kahawa na kushuka
kwenye stuli.
Sparrow akanitazama kwa huzuni.
“Kuna tatizo, Bwana Ryan?”
“Nadhani ni udadisi wa kupitiliza,” nikasema.
“Weka kwenye bili yangu,” nikatoka nje na kuingia mtaani.
Polisi yule mwenye umbile kubwa
akanifuata.
Itaendelea
kesho…
Comments
Post a Comment