- Get link
- Other Apps
Featured Post
Posted by
Maendeleo Vijijini
on
- Get link
- Other Apps
ZILIKUWA ni dola mia
tatu rahisi zaidi ambazo Nelson Ryan ameweza kuzipata, lakini ghafla akagundua
kwamba alikuwa amejiingiza mtegoni. Mwito wa simu, ukionekana hauna kasoro
yoyote, ulimwongoza kwenye mauaji ya binti wa Kichina aliyepiga simu huku
akiongea sana. Simu hiyo pia ikamwongoza moja kwa moja kwenye maisha ya
kihalifu ya Hong Kong. Tangu sasa na kuendelea, Ryan hakuweza kufanya chochote mpaka
atakapompata muuaji ambaye amemwingiza kwenye majanga. ENDELEA…
Hekalu hilo lilikuwa gizani. Niliamini
kwamba hakukuwa na mtu yeyote ndani. Kuhakikisha, nilizunguka nyuma, lakini
hakukuwa na taa zozote.
Nikarejea kwenye gari langu,
nikionekana kufadhaika. Ilionekana kwamba mara tu baada ya mumewe kuelekea
uwanja wa ndege, Bibi Hardwick naye akaondoka nyumbani.
Sikuwa na chochote cha kufanya zaidi
ya kusubiri kwa matumaini kwamba angerejea wakati fulani usiku huo. Huku dola
mia tatu zikiwa katika fikra zangu, nikatulia kusubiri.
Wakati fulani majira ya saa tisa
alfajiri, nikashikwa na usingizi.
Miali ya kwanza ya jua, ikipenya
kwenye kioo cha mbele cha gari iliniamsha haraka. Shingo yangu ilikuwa inauma,
mgongo ulikuwa unauma na hisia za hatia nilipogundua kwamba nililala kwa saa
tatu wakati nilipaswa kuwa macho ili nizivune dola mia tatu.
Mara nikaliona gari la kusambaza
maziwa. Nilimtazama mtu aliyekuwa akisambaza maziwa akisimama na kuanza
kusambaza maziwa katika kila juma. Akaipita nyumba Na. 33, halafu akasimama
jirani na mimi kusambaza maziwa katika nyumba Na. 35.
Alipotoka nje, nikaunga naye.
Alikuwa mtu mzima ambaye uso wake ulionyesha hali ngumu ya maisha na madhira
mbalimbali. Alinitazama kwa macho yanayohoji, akiwa amesimama na chupa zake za
maziwa zikiwa kwenye kikapu alichokishikilia mkononi mwake.
“Umeisahau nyumba Na. 33,” Nilimwambia.
“Kila mtu amepata maziwa lakini siyo Na. 33.”
Alinitazama kuanzia juu, macho yake
ya kizee yakiwa yanadadisi.
“Wanaonekana wako safarini,” alisema.
“Inakuhusu nini, bwana?”
Niliona kwamba alikuwa mtu ambaye
huwezi kuthubutu kufanya naye mzaha. Sikutaka kujiweka katika matatizo ya
kukumbana na polisi hivyo nikachukua kadi yangu ya kazi na kumkabidhi.
Aliichunguza kwa makini, halafu akapiga mluzi wa taratibu akiyabana meno yake,
akarejesha kadi yangu.
“Huwa huleti maziwa kwenye nyumba Na.
33?” Nikamuuliza.
“Hakika huwa naleta, lakini
wamesafiri kwa mwezi sasa.”
“Ni akina nani hao?”
Alilifikiria swali kwa muda.
“Bwana na Bibi Myers.”
“Naamini Bwana na Bibi Hardwick ndio
wanaoishi hapa sasa.”
Aliliweka kapu chini na kuigeuza
kofia yake.
“Kwa sasa hakuna anayeishi hapa,
bwana,” alisema, akijikuna kwenye paji la uso wake. “Ningejua tu kama
angekuwepo mtu pale. Watu lazima wapate maziwa na mimi ndiye ninayewaletea
hapa. Sipeleki maziwa kwenye nyumba Na. 33 kwa sababu hakuna anayeishi pale kwa
mwezi sasa.”
“Hivyo,” nilisema, lakini
sikumaanisha. “Hudhani kwamba Bwana Myers alipangisha nyumba yake kwa mtu huyu?”
“Nimemhudumia Bwana Myers kwa miaka
nane sasa,” aliniambia. “Hajawahi kupangisha nyumba yake kwa mtu yeyote. Daima
husafiri mwezi kama huu kwa mwezi mzima.” Alinyanyua kapu lake. Niliona alikuwa
amechoshwa name na sasa alikuwa anataka kuendelea na kazi yake.
“Humfahamu mtu yeyote anayeitwa John
Hardwick katika eneo hili?” niliuliza bila kuwa na matumaini makubwa.
“Hapa hakuna,” alisema. “Lazima ningejua.
Namfahamu kila mmoja hapa,” huku akitikisa kichwa chake, akaenda kwenye gari
lake na kuelekea nyumba Na. 37.
Uamuzi wangu wa kwanza ulikuwa
kufikiria kama nilikuwa nimeisoma anuani kwa usahihi, lakini najua nilikuwa
makini. Hardwick alikuwa ameandika mwenyewe, zaidi ya kunieleza.
Sasa kwa nini alinilipa dola mia
tatu niketi nje ya jumba ambalo lilikuwa tupu? Pengine msambaza maziwa alikuwa
amekosea, lakini sidhani kama hakuwa sahihi.
Nikarudi kwenye nyumba Na. 33 na
kusukuma mojawapo ya mageti. Katika mwanga wa jua la asubuhi, sikulazimika
kupita uchochoro ule kujiridhisha kwamba jumba lilikuwa jeupe. Madirisha
yalifungwa kwa mbao; kitu ambacho sikukiona usiku wakati wa giza. Jumba
lilikuwa na muonekano wa upweke.
Ghafla zikaja hisia za hatari. Inawezekana
mtu huyu wa ajabu John Hardwick, kwa sababu anazozijua mwenyewe, alikuwa
anataka nimpishe na akanipatia kazi hii kwa sababu hiyo? Siwezi kuamini mtu
yeyote kwa akili zake timamu ambaye angetapanya dola mia tatu ili nimpishe kwa
saa kumi na mbili. Niliona kwamba sikuwa muhimu kiasi hicho, lakini wazo hili
liliendelea kujirudia. Ghafla nikataka kurejea ofisini kwangu haraka kuliko
hata nilivyotamani nioge na ninyoe ndevu na kupata kahawa.
Nilirejea haraka kwenye gari langu
na kuendesha kasi kutoka mlimani. Majira haya hakukuwa na magari mengi na
nikafika ofisini kwangu wakati mshale wa saa ulipogonga saa moja. Baada ya
kuliacha gari, niliingia kwenye jengo ambako mlinzi alikuwa ameshikiliza
ufagio, akipumua kwa kasi na kubeua midomo. Alinitazama kwa jicho kali na
kugeuka. Alikuwa ni mtu aliyemchukia kila mtu, akiwemo yeye mwenyewe.
Nilipandisha hadi ghorofa ya nne na
kutembea haraka kuelekea kwenye mlango maarufu uliokuwa na maandishi meusi:
Nelson Ryan, Mpelelezi.
Nilichukua funguo zangu, lakini kwa
mawazo ya sekunde chache, nikagusa kitasa na kukijaribu. Mlango haukuwa
umefungwa japokuwa niliufunga wakati nikiondoka jana jioni. Niliusukuma mlango
na kutazama ofisi ya nje ambayo ilikuwa na meza ambako kulikuwa na magazeti,
viti vinne vilivyochakaa na kipande cha zuria: mtazamo kwa yeyote mwenye miguu
ya unyenyekevu.
Mlango wa ndani, unaoelekea kwenye
ofisi yangu ulikuwa wazi. Huu pia ulikuwa umefungwa kabla ya kuondoka.
Kwa mara nyingine nikiwa na fikra za
hatari, niliufikia mlango na kuufungua zaidi.
Akiwa ameketi, akinitazama kwenye
kiti cha wateja alikuwa binti mrembo wa Kichina, mikono yake ikiwa imejikunja
ovyo. Alikuwa amevaa gauni aina ya Cheongsam la rangi ya kijani na fedha, likiwa
nimekaa kihasara kama kuonyesha miguu yake mizuri. Alionekana akiwa mwenye
amani na hakuwa na mshtuko. Kutokana na damu kwenye titi lake la kushoto,
nilihisi kwamba alipigwa risasi haraka na bila kutegemea: haraka zaidi, kiasi
kwamba hakuwa na muda wa kuwa na hofu. Yeyote aliyemuua alikuwa amefanya kazi
nzuri ya haraka.
Nikitembea kana kwamba niko majini,
niliingia kwenye chumba na kuugusa uso wake ambao tayari ulikuwa wa baridi.
Alikuawa saa kadhaa nyuma.
Baada ya kuvuta pumzi ndefu,
nikainua simu na kuwapigia polisi.
Itaendelea
kesho…
Comments
Post a Comment