- Get link
- Other Apps
Featured Post
Posted by
Maendeleo Vijijini
on
- Get link
- Other Apps
Na Daniel Mbega
NI mwaka
wa 42 tangu Yanga ilipoifunga Simba kwenye ardhi ya Zanzibar, lakini hali
inaonekana bado ngumu kwani imepoteza tena mchezo wa leo wa nusu fainali ya
Kombe la Mapinduzi.
Kama ilivyokuwa mwaka 1992, Yanga safari hii imetolewa kwa penalty 4-2 baada ya kutoka suluhu katika dakika 90 za kawaida.
Huu ni
mchezo wao wa tano katika uwanja wa Amaan Zanzibar na Jumatatu ya Januari 13,
1975 ndiyo siku pekee ambayo Yanga iliivua ubingwa Simba kwenye Uwanja huo wa
Amaan, baada ya kuichapa mabao 2-0 katika mchezo wa fainali wa Klabu Bingwa
Afrika Mashariki na Kati.
Huo ndio
ushindi wa pekee wa Yanga dhidi ya mahasimu wao katika mechi ambazo zimechezwa
visiwani Zanzibar katika historia yao.
Siku hiyo
Yanga ilipata mabao yake kupitia kwa Sunday Ramadhan Manara ‘Computer’ dakika
ya 16 na Gibson Sembuli dakika ya 85 na kusababisha mgogoro mkubwa ambao
hatimaye ukazaa klabu ya Nyota Nyekundu kutoka ubavuni mwa Simba.
Mgawanyiko
huo ulitokana na vipigo mfululizo na kuvuliwa ubingwa kwa Simba, kwani mbali ya
kuvuliwa ubingwa wa Cecafa mwaka huo, miezi mitano nyuma, yaani Agosti 10,
1974, Yanga ilikuwa imeivua Simba Ubingwa wa Taifa katika pambano la kihistoria
kwenye Uwanja wa Nyamagana jijini Mwanza baada ya kuifunga mabao 2-1 yaliyofungwa
na Sembuli na Sunday Manara katika mechi ambayo hata mashabiki wa Yanga walikuwa
wanaamini wamekwishafungwa.
Katika mechi
ya fainali mwaka 1975, Yanga ilikuwa imeifunga Gor Mahia ya Kenya mabao 2-0
kwenye nusu fainali Jumamosi, Januari 11, wakati Simba nayo iliichapa Mufulira
Wanderers ya Zambia kwa mabao 2-0 Januari 12.
Lakini miaka
17 baadaye, yaani Jumamosi, Februari 15, 1992 usiku, kwenye uwanja huo huo wa
Amaan, Yanga ikashindwa kufanya maajabu kama ya 1975 kwenye mchezo wa fainali
pia ya Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati baada ya kufungwa kwa matuta na
Simba.
Simba
iliifunga Yanga kwa mikwaju ya penalty 5-4 (ushindi wa jumla wa 6-5) baada ya
kutoka sare ya bao 1-1 kwa muda wa dakika 120, mabao ambayo hata hivyo
yalipatikana katika kipindi cha dakika 90.
Mlinzi wa kulia
wa Yanga, David Mwakalebela, ndiye aliyeikosesha timu yake penalty hiyo na
Simba ikafanikiwa kutwaa ubingwa. Hiyo ilikuwa ni penalty ya nane ambapo Salum
Kabunda ‘Ninja’, Said Mwamba ‘Kizota’ na Abubakar Salum ‘Sure Boy’ nao pia
walikosa kwa Yanga.
Kwa upande
wa Simba, waliokosa ni Twaha Hamidu ‘Noriega’, Kassongo Athumani Mgaya na
Damian Morisho Kimti.
Wafungaji
wa penalti za Simba walikuwa George Masatu, Hamza Maneno, Fikiri Magosso, Issa
Kihange na George Lucas na walioifungia Yanga ni Said Mwabambe ‘Zimbwe’, Issa
Athumani, Sanifu Lazaro ‘Tingisha’ na
Hamisi Gaga ‘Gagarino’.
Yanga
ilibaki na wachezaji 10 kwa dakika 89 kati ya 120 za mechi hiyo baada ya
Kenneth Mkapa kutolewa kwa kadi nyekundu katika dakika ya 31.
Bao la
Simba lilifungwa na Hussein Marsha katika dakika ya 54 akiunganisha krosi ya
Twaha Hamidu, na Kizota ndiye aliyeisawazishia Yanga katika dakika ya 63.
Siku hiyo,
timu zilipangwa hivi: Simba:
Mohammed Mwameja, Kassongo Athumani, Twaha Hamidu, Fikiri Magosso, George
Masatu, Ramadhan Lenny/Hamza Maneno, Michael Paul/Issa Kihange, Hussein Marsha,
Gebo Peter, Damian Kimti na George Lucas.
Yanga: Steven Nemes, Joseph Lazaro, Kenneth Mkapa,
Salum Kabunda, Said Zimbwe, Issa Athumani, Sanifu Lazaro, Hamis Gaga, Zamoyoni
Mogella/Abubakar Salum, Said Mwamba Kizota na Thomas Kipese/David Mwakalebela.
Mechi nyingine
iliyofanyika kwenye uwanja huo wa Amaan, Zanzibar baina ya Yanga na Simba
ilikuwa katika Ligi Kuu ya Muungano, Jumanne, Oktoba 27, 1992 ambapo bao la
Damian Morisho Kimti la dakika ya 21.
Siku hiyo
timu zilikuwa na: Yanga: Stephen
Nemes, David Mwakalebela, Kenneth Mkapa, Salum Kabunda, Said Mwaibambe
'Zimbwe', Willy Mtendawema, Justine Mtekere/Abubakar Salum, Steven Mussa, Said
Mwamba, Issa Athumani na Thomas Kipese/Abeid Mziba.
Simba: Mohammed Mwameja, Kassongo Athumani, Twaha
Hamidu, Iddi Selemani, Fikiri Magosso, Ramadhan Lenny, Bakari Iddi/Ayoub Mzee,
Hussein Marsha, Gebo Peter, Damian Kimti na George Lucas.
Mara ya
nne kwa mahasimu hao kukutana Zanzibar ilikuwa Jumatano, Januari 12, 2011
katika mchezo wa fainali ya Kombe la Mapinduzi, ambao ulishuhudia Yanga
wakilala kwa mabao 2-0 ambayo yalifungwa na Mussa Hassan Mgosi dakika ya 33 na
Shija Mkina dakika ya 71.
Leo hii
wamekumbana katika nusu fainali ya Kombe hilo la Mapinduzi ikiwa ni mara yao ya
tano katika kihistoria kucheza Visiwani Zanzibar, lakini imeonekana kwamba
Yanga bado haijapata dawa ya ushindi dhidi ya Simba visiwani humo.
Mkosi wa
Yanga ulijitokeza kuanzia kwenye mchezo wa mwisho wa Kundi B Jumamosi ya
Januari 7, 2017 wakati ilipokubali kipigo cha aibu cha mabao 4-0 kutoka kwa
Azam FC.
Yanga wakati
huo ilikuwa imeanza vizuri kwa kuifunga Jamhuri ya Pemba mabao 6-0 na kuilaza
Zimamoto 2-0, mwendokasi ambao ulipunguzwa na Azam na kuangukia nafasi ya pili
kwenye kundi hilo.
Simba wao
waliongoza Kundi A baada ya kushinda 2-1 dhidi ya Taifa Jang’ombe, 1-0 dhidi ya
KVZ, sare ya 0-0 na mabingwa watetezi URA na kuifunga Jang’ombe Boyz 2-0.
Vikosi vya
leo vilikuwa; Yanga: Deogratius
Munishi ‘Dida’, Juma Abdul, Mwinyi Hajji, Andrew Vincent ‘Dante’, Kelvin
Yondan, Saidi Juma ‘Makapu’, Simoni Msuva, Thabani Kamusoko, Amissi Tambwe,
Haruna Niyonzima na Deus Kaseke.
Simba: Daniel Agyei, Janvier Bokungu, MOhammed Hussein
'Tshabalala', Abdi Banda, Method Mwanjali, Jonas Mkude, Shiza Kichuya, James
Kotei, Juma Luizio, Muzamil Yassin na Mohamed Ibrahim.
Comments
Post a Comment