- Get link
- Other Apps
Featured Post
Posted by
Maendeleo Vijijini
on
- Get link
- Other Apps
JAMHURI
YA MUUNGANO WA TANZANIA
WIZARA
YA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO
TAARIFA
KWA UMMA
TAHADHARI
KUHUSU UGONJWA WA MAFUA YA NDEGE ULIOONEKANA KATI YA JAMII YA NDEGE PORI KATIKA
NCHI JIRANI YA UGANDA JANUARI 2017.
Wizara ya Afya,
Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto inapenda kutoa taarifa kwa umma,
kuhusu kuwepo kwa virusi vya mafua makali ya ndege katika nchi jirani ya
Uganda.
Aidha taarifa hiyo
imeeleza kuwa maeneo yalioathirika ni maeneo yanayozunguka ziwa Victoria pamoja
na ziwa lenyewe. Ugonjwa huu umengundulika baada ya kuwepo kwa vifo vingi vya
ndege pori katika maeneo ya Lutembe beach, Masaka, Kachanga, Bukibanga na
Bukakata ya nchini Uganda. Vilevile, vifo hivi vimetokea kwa baadhi ya ndege
wafugwao (kuku na bata) na inahisiwa kuwa ndege hao wamepata virusi vya ugonjwa
huo kutoka kwa ndege pori wanaohama kutoka nchi za Ulaya. Vifo hivyo vya ndege
pori vilianza kuonekana tangu tarehe 2 Januari, 2017 na vimeonekana kuendelea hadi
sasa. Kwa hapa nchini Tanzania hakuna vifo vya ndege vilivyoripotiwa hadi sasa.
Kwa kuwa hadi sasa
hakuna binadamu yeyote aliyeonekana kuwa na dalili za ugonjwa huo huko nchini
Uganda, tahadhari inatolewa kwa kuwa kuna uwezekano mkubwa wa ugonjwa
kusambaa kwa binadamu ikiwa hatua madhubuti za kujikinga hazitazingatiwa.
UGONJWA WA MAFUA YA
NDEGE
Ugonjwa huu
unasababishwa na virusi vya aina ya “Influenza” na huenezwa na ndege pori
wanaohama hama (Migratory birds). Ndege hawa hubeba virusi vya ugonjwa huu bila
ya kuonesha dalili za ugonjwa, hivyo huweza kuambukiza ndege wanaofugwa
majumbani mfano kuku na bata wakati wanapokutana nao. Aidha ndege hao huweza
kuambukiza ugonjwa huu kwa kupitia njia ya kinyesi ambacho hudondoshwa ardhini
au kwenye mabwawa na madimbwi ya maji.
Binadamu anaweza
kuambukizwa ugonjwa huu kwa kugusana na ndege au kinyesi cha ndege
aliyeathirika na ugonjwa huu. Hivyo ni muhimu kutokugusa mizoga ya ndege pori
au kinyesi chake. Maambukizi ya ugonjwa huu yanaweza pia kutoka kwa ndege pori
na kuathiri jamii ya kuku na bata na ndege ambao wanafugwa nyumbani. Hivyo
wananchi wanaombwa pia kutoa taarifa iwapo wataona dalili zozote za ugonjwa na
vifo katika jamii ya ndege hawa wa kufugwa pamoja na ndege pori. Aidha,
iwapo kutakuwa na maambukizi kwa jamii ya ndege hawa wa kufugwa, binadamu
anaweza pia kupata maambukizi wakati wa kuchinja kuku, kunyonyoa manyoya, na
wakati wa kutayarisha kabla ya kumpika.
Vilevile kuna
uwezekano wa virusi hivi kuambukizwa kutoka kwa binadamu mwenye uambukizo
kwenda kwa binadamu mwingine na hii ikitokea inaweza kusababisha mlipuko mkubwa
unaoweza kusambaa pande zote za dunia (Influenza Pandemic).
Maambukizi ya binadamu
kwenda binadamu mwingine hutokea kwa njia ya kugusana na maji maji ya kutoka
njia ya hewa iwapo mgonjwa atakohoa au kupiga chafya bila kufunika pua au
mdomo, au kwa njia ya kugusa sehemu zenye virusi zilizochafuliwa na mgonjwa na
mtu huyo kujigusa mdomomi au puani.
Dalili za ugonjwa wa
mafua ya ndege ni pamoja na; homa kali, kutokwa na makamasi mepesi pamoja
na mafua, kuumwa na kichwa, kukohoa, vidonda kooni, kupumua kwa shida na
vichomi. Vilevile baadhi ya wagonjwa wanaweza kuwa na dalili kama kuharisha,
kutapika, kuumwa na tumbo na kutokwa na damu puani na kwenye ufizi.
HATUA ZINAZOCHUKULIWA
NA WIZARA KATIKA KUZUIA UGONJWA HUU USIINGIE NCHINI
Kuanzia mwaka 2007,
nchi yetu imekuwa katika tahadhari ya ugonjwa wa mafua makali ya ndege na
iliandaa Mpango Mkakati wa Kuzuia na kudhibiti ugonjwa wa mafua makali ya
Ndege, ambao ndio ulitumika kuboresha utayari wa nchi na kuweza kufanikisha
kudhibiti mafua makali ya nguruwe yaliyokuwa tishio duniani mwaka 2009. Aidha,
mnamo mwaka 2012, Wizara kwa kushirikiana na Sekta za Mifugo, Maliasili na
Taasisi za Utafiti za NIMR na TAWIRI, chini ya uratibu wa Ofisi ya Waziri Mkuu
iliweza kuandaa Mpango Mkakati wa miaka 5 wa Kudhibiti na Kuzuia magonjwa ya
binadamu yanayoweza kutoka kwa wanyama, na mpango huu unatekelezwa hadi sasa.
Kufuatia tishio la ugonjwa huu , mpango huu utatumika pia katika kutekeleza
afua zilizoanishwa ili udhibiti ugonjwa huu usiingie nchini.
Vile vile hatua
zifuatazo zimechukuliwa baada ya kupata taarifa ya tahadhari ya ugonjwa huu
hapo jana 16 Januari 2017;
Kushirikiana na ofisi
ya uratibu wa magonjwa yanayowapata binadamu na wanyama (Zoonotic Diseases)
iliyoko chini ya ofisi ya Waziri Mkuu (One Health Coordination Office), ambapo
mkutano maalum umepangwa kufanyika tarehe 18 Januari 2017 ili kuweza
kukutanisha wadau wote na hivyo kuandaa Mpango kazi wa namna ya kuzuia na
kudhibiti ugonjwa huu.
Barua za tahadhari za
ugonjwa huu zimepelekwa kwa Makatibu Tawala wa mikoa yote ya Tanzania Bara
pamoja na . Fact Sheet (Ainisho Sanifu) za namna ugonjwa huu unavyoweza
kuenezwa, kudhibitiwa pamoja na namna ya kutambua ugonjwa huu
Kupitia kwa Waganga
Wakuu wa Mikoa na Wilaya, Wizara imetoa maelekezo ya kuimarisha mfumo wa
ufuatiliaji na utambuzi wa magonjwa (Surveillance) katika vituo vya kutolea
huduma nchini kote. Aidha katika vituo maalum ambapo ufuatiliaji wa karibu
umekuwa unafanyika kwa miaka kadhaa sasa, yaani katika mikoa ya Mwanza, Kigoma,
Arusha, Manyara, Dodoma, Dar es salaam na Mtwara, tumeimarisha usimamizi wa
ufuatiliaji wa karibu na kuelekeza kuwa kwa sasa wagonjwa wote wanoonekana kuwa
na dalili zinazofanana na mafua makali ya influenza wachukuliwe sampuli ambazo
zitapimwa kwenye maabara ya Taifa ya NHLQATC ambayo ina uwezo wa kufanya
utambuzi huo.
Kuimarisha ufuatiliaji
wa ugonjwa pia katika viwanja vya ndege, mipakani pamoja na bandari ili kubaini
wagonjwa waingiao nchini wakiwa na dalili za ugonjwa huo.
Wizara pia inaandaa
Timu kwa kushirikiana na Wizara ya Mifugo ili timu hii ya Taifa iweze kwenda
kujenga uwezo wa kamati za kudhibiti milipuko ya mgonjwa na majanga hususani
kwenye mkoa wa Kagera na mkoa wa Mwanza. Aidha Timu hii pia itashirikiana
na Timu za Mikoa kuandaa Mpango Mkakati wa Kudhibiti Ugonjwa huu usiingie ikiwa
ni pamoja na kuainisha maeneo ya kuboresha ikiwemo upatikanaji wa vifaa kinga
(Personal Protection Equipment, PPE)
Ili kudhibiti kuenea
kwa ugonjwa huu jamii inaaswa kuzingatia yafuatayo:
Kutoa taarifa endapo
wataona kutokea kwa vifo vya ndege pori au wafugwao (kuku, bata na
wengineo) kwa wataalamu wa mifugo, afya au ofisi ya serikali iliyo karibu nawe
Kutokugusa mizoga au
ndege wagonjwa bila kutumia vifaa kinga
Kuepukana na tabia ya
kuishi nyumba moja na ndege wafugwao
Kuepuka kuchinja kuku
au bata wanaoonyesha dalili yoyote ya ugonjwa
Kunawa mikono vizuri
kwa kutumia sabuni
Kupika nyama au mayai
ya ndege kwa muda mrefu usiopungua nusu saa. .
Kuepuka kushika ndege
wa porini na ndege wa majumbani wanaohisiwa kuwa na ugonjwa huu.
Hitimsho
Serikali inasisitiza
kuwa mpaka sasa ugonjwa wa mafua ya ndege haujaingia hapa nchini ila upo katika
nchi jirani ya Uganda katika jamii ya ndege pori kwa sasa. Kwa kuwa magonjwa
hayaangalii mipaka, tunahitaji kuchukua tahadharii madhubuti ili kuzuia ugonjwa
huu usiingie hapa nchini. Hivyo Wananchi wanahimizwa kuzingatia kanuni za afya
za kuzuia ugonjwa huu ikiwa ni pamoja na kutoa taarifa mara moja waonapo vifo
vya ndege au kuku. Pia wanatakiwa kuripoti haraka kwenye vituo vya kutolea
huduma za afya mara waonapo dalili zozote za ugonjwa huu. Vile vile wananchi
wanatakiwa kutokuwa na hofu kwani Serikali imejiandaa na itachukua hatua madhubuti
za kudhibiti ugonjwa huu.
Mhe. Ummy Mwalimu (Mb)
Waziri wa Wizara ya
Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, wazee na Watoto.
Tarehe 18 Januari,
2017
Comments
Post a Comment