- Get link
- Other Apps
Featured Post
Posted by
Maendeleo Vijijini
on
- Get link
- Other Apps
Na Daniel Mbega
CHAMA cha
Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kimeparaganyika huku vijana ‘wanaharakati’ wa
chama hicho wakiwa wamekata tamaa.
Naam. Huo ndio
ukweli wenyewe ingawa wahusika hawataki kuukubali.
Kutoweka kwa
mwanasiasa kijana msomi Bernerd Rabiu Saanane – iwe kwa kufichwa, kutekwa ama ‘kujiteka’
mwenyewe – na kutemwa kwa makamu mwenyekiti wa Baraza la Vijana Chadema
(Bavicha), Patrick ole Sosopi katika kinyang’anyiro cha uchaguzi wa mwenyekiti
wa Kanda ya Nyasa hivi karibuni kumeibua mambo mengi ambayo wenyewe walikuwa
wanayaficha.
Mojawapo ya
mambo hayo, kwanza, ni kudhihirisha kuwa uongozi wa juu wa Chadema hauwajali
vijana na unawatumia kwa ajili tu ya harakati zao za kukidhi matakwa binafsi ya
viongozi.
Suala la
Ben Saanane kushindwa kushughulikiwa wala kuzungumziwa na viongozi wa juu,
akiwemo Mwenyekiti wake Taifa, Freeman Mbowe, ni mfano hai kwamba uongozi
ulikuwa unamtumia kijana huyo kwa ajili tu ya harakati na siyo kuthamini
mchango wake.
Haijuzu kuona
Mbowe akishindwa kuzungumza ama kushughulikia suala la msaidizi wake huyo wa
karibu ambaye duru za ndani ya Chadema zinasema ndiye aliyetumika kuwaondoa ‘wanachama
wakorofi’ kama Zitto Kabwe kiasi cha kutuhumiwa kutaka kumlisha sumu, na
akatumika pia kumrekodi kwa siri Dk. Wilbrod Slaa, wakati akiwa Katibu Mkuu wa
chama hicho kwa kinachotajwa kuwa ‘maelekezo ya Mbowe’.
Leo hii
Mbowe akiulizwa, kwa haki ya Mwenyezi Mungu, kama alikuwa hata anapafahamu
mahali alikokuwa akiishi Ben Saanane, hawezi kutoa jibu sahihi kwa sababu ni
ukweli kwamba hajui wapi alikokuwa akiishi japokuwa ni msaidizi wake.
Siyo lazima
kujua mahali anakoishi kila mwanachama, lakini kwa mtu wako wa karibu, ambaye
ndiye anayekushauri ama kukuandalia hata hotuba, hakika ni jambo la ajabu
kutojua makazi yake.
Si hivyo
tu, kutoweka kwa Ben pia kumefichua ukweli kwamba, hata viongozi wenyewe wa juu
hawajuani makazi yao – yaani Mwenyekiti Mbowe hajui hata anakoishi Katibu Mkuu
wake Mashinji na ni hivi majuzi tu ameweza kujua nyumbani kwa Mwanasheria Mkuu
wa chama hicho, Tundu Lissu.
Leo hii
Mbowe hajui mahali anakoishi John Mnyika, kijana mahiri ambaye kwa miaka zaidi
ya 10 amekuwa mtu muhimu katika harakati za chama hicho. Hiki ni chama cha
kihuni. Chama cha ‘wapiga dili’!
Hii maana
yake ni kwamba, wanasiasa hao wa kiharakati hukutana tu kila panapokuwa na
jambo la kulizungumzia, lakini siyo chama kilicho na mtazamo wa kujenga umoja
wa kidemokrasia unaoonyesha kujali ustawi wa kijamii, achilia mbali kutambua
makazi ya wanachama wengine.
Kitendo
cha Mbowe kwenda Mbeya na jina la Mchungaji Peter Msigwa mfukoni kama ndiye ‘chaguo
lake’ kwa nafasi ya uenyekiti wa Kanda ya Nyasa kimewavunja moyo vijana wengi
wanaharakati, ambao walijiunga na Chadema kwa mihemko na kutumika kuwanufaisha
wengine.
Na vijana
hao wengi wao wanajuta kwa kuingia kwenye harakati – bila hata kujua siasa ni
nini – na kuachana na taaluma zao kwa matarajio makubwa kwamba wengeweza kupata
nafasi ikiwa Chadema ingeingia madarakani. Wamekata tamaa.
Kile ambacho
wapinzani walikuwa wakikisema kuhusu Chama cha Mapinduzi (CCM) kwamba ni ‘chama
cha wajanja wachache’ ndicho kinachoendelea ndani ya Chadema.
Kwamba wewe
kama ‘siyo mtu wao’ hata upige kelele namna gani katu hutaweza kupata nafasi.
Tatizo
kubwa la Chadema kwa sasa ni kutokubali kwamba kuna tatizo na kimekuwa kama
jabali ambalo kubadilika kwake ni lazima ugonge kwa nyundo, au kama mlima,
ambao mabadiliko yake ni ama miti kunyauka ama mvua itakayostawisha misitu na
kuombea wasitokee ‘wakata mkaa’ wakaifyeka.
Wanaodhani
Chadema imepoteza mwelekeo kwa sababu ya kulamba matapishi yao kwa ‘kumtakasa’ Edward
Lowassa, mtu waliyemhubiri kuwa miongoni mwa watu 11 wanaoitafuna Tanzania,
wako sahihi lakini wanashindwa kujua kiini hasa ni nini.
Kwa miaka
takriban 7, Chadema ilihubiri kila kona kwamba Lowassa ni fisadi na kwa hakika
walikuwa wakijiandaa kuigaragaza CCM ikiwa ingempitisha Lowassa kuwania urais
kama alivyokaririwa Mbowe mnamo Mei 29, 2015 akisema kwamba waziri mkuu huyo wa
zamani hakuwa na uwezo wa kupambana na ufisadi na kwamba alikuwa dhaifu.
Msimamo
waliokuwa nao kupitia Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) ulivurugwa kwa
makusudi na Chadema, ambapo miezi miwili baadaye Mbowe huyo huyo akamkaribisha
kwa huba na bashasha Lowassa na kumkabidhi ‘mikoba’ ya kuwania urais ambayo
awali walikuwa wameazimia kumpatia Padri Dk. Wilbrod Slaa.
Kilichowafanya
‘wabadili gia angani’ wanakijua wenyewe, na baadhi ya wananchi wanaweza kuamini
tetesi zilizozagaa tangu wakati wa kampeni kwamba vigogo hao wa Chadema na
Ukawa kwa ujumla walipokea kitita cha fedha kutoka kwa Lowassa ndiyo maana
wakachukua jukumu la ‘kumtakasa’ na kumpa nafasi ya kuwania urais.
Kitendo
cha kumkaribisha Lowassa na ‘masalia’ ya CCM, wengi wao wakiwa ni wale
walioanguka kwenye kura za maoni, na uamuzi wao wa ‘kufunika’ tuhuma za ufisadi
za kiongozi huyo huku wakitumika kama ‘wapiga filimbi wa Hamelin’ siyo tu kiliwapunguzia
sifa Chadema, bali kiliwadhoofisha hata Ukawa kwa ujumla wake ingawa itakuwa
vigumu kwa wengi kuamini hilo.
Ushindi
ambao upinzani imeupata katika uchaguzi mkuu haukutokana na chama kimoja, bali
umekuja kutokana na nguvu ya umoja waliokuwa wameuunda, vinginevyo ukihesabu
kwa chama kimoja kimoja, Chadema ingeweza kuambulia patupu.
Tatizo
kubwa la Chadema ni kutokubali mabadiliko ya kidemokrasia ingawa chama hicho
kinajiita ni ‘cha demokrasia’.
Leo hii
kila anayetoa maoni ya kukijenga chama, ikiwa tu atamkosoa Mbowe, basi ni
aidui.
Mbaya zaidi
ni kwamba, Chadema imeamua kumtosa hata muasisi wake, Mzee Edwin Mtei, kwa
sababu tu aliwahi kukosoa mfumo wa uongozi! Leo hakuna anayejali kuhusu mzee
huyo.
Chadema
iliharibika baada ya kuondoka kwa Bob Nyanga Makani kwenye nafasi ya uenyekiti
na kuingia kwa Mbowe, ambaye mwaka 2005 alisimama kukiwakilisha chama hicho
katika mbio za urais ikiwa ni mara ya kwanza tangu uchaguzi mkuu wa kwanza wa
vyama vingi ulipoanza mwaka 1995.
Licha ya
kushindwa katika uchaguzi huo, lakini bado Mbowe aliamini kwamba anao uwezo
mkubwa wa kukiongoza chama hicho, lakini tatizo la udini na ukanda likaanza
kukiandama chama.
Madai
yaliyotolewa na aliyekuwa Makamu Mwenyekiti wa chama hicho, Chacha Zakayo
Wangwe, mwaka 2008 na kumfanya asimamishwe uanachama, kama yangalishughulikiwa
kwa tuo yangeweza kuliondoa ombwe ambalo bado lingali linakitafuna chama hicho.
Wangwe
alipingwa vikali kwamba ndani ya chama hicho hakukuwa na makundi wala ukanda,
lakini hata wakati mauti yanamfika alikuwa anatoka Dodoma kuja Dar es Salaam
kwa lengo la kujieleza kwenye Kamati Kuu kuhusu tuhuma alizozitoa. Mauti
yakamnyamazisha ghafla!
Madai ya
udikteta, ukanda na ukabila ndani ya chama hicho yalishika kasi zaidi mwaka
2009 wakati aliyekuwa Naibu Katibu Mkuu (Bara), Zitto Zuberi Kabwe,
alipotangaza kujitosa kuwania uenyekiti.
Ikaelezwa
kwamba muasisi wa chama hicho, Edwin Mtei, alimwita kijana huyo na kumuomba
aachane na ndoto za kushindana na mwenyekiti wake.
Lakini
licha ya kuacha huku akilalamika chama hicho kuendeshwa kwa ukanda, bado
‘bakora’ za kumwadhibu kwa kosa hilo la kutaka kuwania uenyekiti hazikukoma na
zaidi akaanza kutiliwa fitina kwa kila jambo alilolifanya.
Fimbo
nzito zaidi ilijitokeza mwaka 2013 wakati Zitto kwa mara nyingine alipotangaza
kwamba iwe isiwe lazima agombee uenyekiti.
Bila kujua
kwamba tayari kulikuwa na mkakati wa kummaliza kijana huyo, akajikuta
akifukuzwa uanachama kwa maelezo kwamba alikuwa amepanga njama za kumpindua
Mbowe akiwatumia baadhi ya wanachama vijana.
Tumeshuhudia
pia hata baada ya Dk. Slaa kujiengua kwenye chama hicho, ambapo alizushiwa
mambo mengi na kuambiwa kwamba amehongwa na CCM.
Dk. Slaa,
kama ilivyokuwa kwa aliyekuwa Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF) Profesa
Ibrahim Haruna Lipumba, aliamua kujiengua akipinga uamuzi wa mwenyekiti wake wa
‘kumkaribisha’ Lowassa ambaye walimwita fisadi.
Doa la
kashfa ya uteuzi wa wabunge wa viti maalum bado halijafutika huku Mbowe
akituhumiwa kumpendelea mzazi mwenziwe, Joyce Mkya, kwenye ubunge wa viti
maalum pamoja na wapendwa wengine wa viongozi wa juu wa chama badala ya wale
waliotoa mchango mkubwa.
Kwa hiyo,
ikiwa kweli Chadema wanataka kukisuka chama hicho, wanapaswa kuondoa ukanda na
ukabila, na zaidi chama kinaweza kuimarika mara atakapoondoka Mbowe kwenye
nafasi ya uenyekiti.
Ikiwa
kweli chama hicho kinataka kusimama, basi lazima wafanye mabadiliko makubwa,
kwa sababu kujipanga kwao kwa ajili ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2020 hakutakuwa
na maana yoyote kwa sababu hoja ya uwajibikaji na vita dhidi ya ufisadi
inatekelezwa kwa kasi ya ajabu na Rais Magufuli ambaye siyo tu anapongezwa na
wananchi wote, bali hata viongozi wa mataifa ya nje na kama kuna mpinzani
anampinga, basi huyo ni ‘mjeuri’.
0656-331974
www.brotherdanny.com
Comments
Post a Comment