Featured Post

SALAMU YA MAALIM SEIF YABAMBA MITANDAONI NCHINI

By Joyce Mmasi, MwananchiDar es Salaam. Picha inayomuonyesha Maalim Seif Sharrif Hamad akiwa ameinama mikono ikiwa tumboni, huku Rais wa Zanzibar, Dk Ali Mohamed Shein akiwa amenyoosha mkono kuashiria kutaka kusalimiana na katibu huyo mkuu wa CUF, sasa imekuwa moto mtandaoni.
Picha hiyo ilichukuliwa wakati wa shughuli za mazishi ya Rais wa Pili wa Zanzibar, Aboud Jumbe Mwinyi kisiwani humo mapema wiki hii, na sasa inaigizwa na watu wa kariba tofauti wanaotuma mitandaoni picha inayofanana na tukio hilo.
Picha hizo zinaonyesha watoto, vijana na hata watu wa makamo wakiigiza tukio hilo.
Wawili hao walipambana kwenye Uchaguzi Mkuu wa Rais wa Zanzibar uliofutwa na mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi (ZEC), Jecha Salim Jecha Oktoba 28, siku ambayo alitakiwa atangaze mshindi wa mbio za urais. CUF ilisusia uchaguzi mpya uliotangazwa na Jecha.
Vitendo hivyo vya kuigiza matukio ya watu muhimu sasa vimepamba moto mitandaoni. Miongoni mwa matukio yaliyoigwa sana mitandaoni ni la waziri wa zamani wa kilimo, Steven Wasira kupiga picha akiwa hajafunga vizuri vifungo vya koti na Rais wa Zimbabwe, Robert Mugabe kudondoka.
Pia tukio jingine lililoigwa sana ni la Rais wa Uganda, Yoweri Museveni kuonekana amekaa kwenye kiti pembeni ya barabara akiongea na simu huku msafara wake ukiwa unamsubiri.
CHANZO: MWANANCHI

Comments