Featured Post

DC MTATURU: SERIKALI IPO TAYARI KUCHUKIWA NA WAVIVU

Mkuu wa Wilaya ya Ikungi Mirajji Jumanne Mtaturu akisisitiza jambo wakati wa kufunga mafunzo ya waendesha pikipiki.

Mkurugenzi wa Taasisi inayojihusisha na kupunguza umasikini na kutunza mazingira nchini Tanzania (APEC), Respicius Timanywa akiwashukuru washiriki wote wa mafunzo hayo
Dc Mtaturu (Kushoto) akimkabidhi Mkurugenzi wa APEC Respicius Timanywa zawadi ya kuku iliyotolewa na wahitimu wa mafunzo hayo
Mkuu wa Wilaya ya Ikungi Mirajji Jumanne Mtaturu akisisitiza juu ya umuhimu wa mafunzo ya usalama barabarani.
Dc Mtaturu akionyesha kuku aliyokabidhiwa kama zawadi baada ya kukubali kuwa mgeni rasmi  wakati wa kufunga mafunzo hayo
Baadhi ya washiriki wa mafunzo ya elimu ya usalama barabarani wakionyesha alama za barabarani walizozichora wao wenyewe kwa ajili ya kuashiria kuelewa mafunzo waliyopatiwa
Baadhiya Bodaboda za washiriki zikiwa zimepaki bila kufanya kazi ya kubeba abiria ambapo wamiliki walikuwa kwenye mafunzo



Na Mathias Canal, Singida
Serikali imeeleza kuwa ipo tayari kuchukiwa na wananchi wavivu wasiotaka kujishughulisha na Ujasiriamali, Kilimo, Uvuvi, Ufugaji na Biashara ili kukuza pato la kaya zao.

Hayo yamesemwa na Mkuu wa Wilaya ya Ikungi Mhe Miraji Jumanne Mtaturu wakati wa kufunga mafunzo ya usalama Barabarani kwa Waendesha pikipiki maarufu kama Bodaboda wa Wilaya ya Ikungi yaliyohusisha Kata ya Issuna na na Kata ya Mkiwa na kufanyika JMC Hotel Kijijini Issuna B.

Katika mafunzo hayo yaliyochukua siku sita yamewakutanisha pamoja waendesha Bodaboda 84 ambao wamefundishwa Alama na sheria zote za usalama Barabarani, Upatikanaji wa leseni, Faida za kulipa kodi na somo la ujasiriamali, Polisi jamii, Ulinzi shirikishi na elimu juu ya maambukizi ya Virusi Vya Ukimwi (VVU) na Ukosefu wa Kinga Mwilini (UKIMWI).

Akiwahutubia wananchi hao Mtaturu amemshukuru Rais wa awamu ya nne Dkt Jakaya Mrisho Kikwete kwa kuanzisha ajira ya pikipiki kwani kwa kiasi kikubwa imesaidia kupunguza uhalifu na kuandaa ajira kwa vijana wengi nchini hivyo kuachana na kujihusisha na mambo yasiyo na tija kwa jamii ikiwemo kushinda vijiweni.

Amesema kuwa mafunzo hayo yanayotolewa na shirika lisilo la kiserikali la APEC yatasaidia kupunguza ajali za pikipiki zinazosababishwa na uzembe wa baadhi ya waendesha pikipiki katika Wilaya zote za Mkoa wa Singida.

Dc Mtaturu amemwagiza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Ikungi kwa kushirikiana na Mkuu wa Polisi Wilaya kuhakikisha madereva Bodaboda waliokwepa mafunzo ya awamu hii wanasajiliwa ili wahudhurie mafunzo yatakayorudiwa kwa awamu ya pili kwa Wilaya nzima, hivyo kwa wale ambao hawatapata mafunzo hawataruhusiwa kuendesha pikipiki zao ili kuepusha ajali mpaka pale watakapopata mafunzo.

“Dereva bila elimu ni sawa na bunduki bila risasi, hivyo nakuagiza mkuu wa Polisi kutowakamata kwa kosa la kutokuwa na leseni angalau kwa kipindi cha miezi miwili wakati wanafuatilia leseni zao”  Alisema Mtaturu

Akizungumzia kuhusu alama za barabarani Mtaturu alisema kuwa tayari ameshamwagiza Mhandisi wa Ujenzi wa Halmashauri kufanya mawasiliano na wakala wa barabara katika maeneo yote ambapo alama za barabarani hazipo.

Ili kuvunja makusudi makusudi ya kuvunja sheria Mkuu huyo amemuagiza Mkuu wa Polisi Wilaya (OCD) amuelekeze mkuu wa Trafiki Wilaya (DTO) ambapo alisema kuanzia leo kila dereva wa pikipiki anapaswa kutembea na kivuli cha cheti na leseni. 

Akisoma risala iliyoandaliwa na wahitimu wa mafunzo ya udereva wa pikipiki Kata ya Mkiwa na Issuna Yohana Chawenda amezitaja changamoto zinazowakabili waendesha bodaboda hao kuwa ni pamoja na kukabwa na kuibiwa pikipiki zao, Upatikanaji wa leseni, baadhi ya abiria kukataa kuvaa kofia ngumu, Baadhi ya waendesha pikipiki kukataa kushiriki mafunzo ya usalama barabarani, Baadhi ya wananchi kuharibu alama za barabarani na Baadhi ya maafisa wa usalama Barabarani kusimamisha pikipiki sehemu isiyo rasmi jambo ambalo linachangia kuongezeka kwa ajali za barabarani.

Mkurugenzi wa Taasisi inayojihusisha na kupunguza umasikini na kutunza mazingira nchini Tanzania (APEC), Respicius Timanywa, amesema kuwa lengo la Taasisi hiyo kutoa mafunzo hayo ni kupunguza ajali na kuwaandaa vijana kujihusisha na ujasiliamali wa uendeshaji wa Bodaboda huku wakiwa katika hali ya usalama.

Timanywa amesema kuwa mafuzno hayo yataendelea katika maeneo mengine ili kutoa fursa kwa watanzania wote wanaopenda kushiriki kwa ajili ya kujifunza kwa manufaa ya leo na kesho.

Zaidi sana amesema kuwa mafunzo hayo pia yamelenga kuwafanya vijana waweze kumiliki fursa kubwa na kutengeneza faida kubwa iliwaweze kulipa ushuru na kodi za serikali.

Comments